Kundi la Saiga lalamikiwa kwa kubomoa nyumba za wananchi Nyamongo

Baadhi ya wakazi wa mji mdogo wa Nyamongo wilaya ya Tarime mkoani Mara wameanza kuyakimbia makazi yao na wengine kulazimika kulala nje na familia zao nyakati za usiku, baada ya nyumba zao kadhaa kubomolewa na kundi la vijana wa Kikurya maarufu kama Saiga linalodaiwa kutekeleza vitendo vya uhalifu, vikiwemo vya uporaji wa mali na fedha kwa mwavuli wa polisi jamii.

Ripota wetu amefika katika eneo la Nyamongo na kushuhudia baadhi ya nyumba zinazodaiwa kubomolewa na kikundi hicho cha Saiga ambacho kilianzishwa kwa nia njema na jeshi la polisi kanda maalum ya Tarime/Rorya katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu,yakiwemo matukio ya mauaji,unyang’anyi wa kutumia silaha na kujeruhi, lakini kwa hivi sasa kikundi hicho kimeacha majukumu yake ya msingi na kuamua kujichukulia sheria mkononi ambapo watuhumiwa wa uhalifu huo wanasemekana kutorokea nchi jirani ya Kenya.

Viongozi wa dini katika eneo hilo la North Mara wamelitaka jeshi la polisi kuacha kufumbia macho vitendo vya kihalifu vinavyohatarisha amani katika jamii kwa kisingizio cha mila kwani kundi hilo la Saiga haliko juu ya sheria na pia hakuna mila inayoruhusu kikundi cha watu kubomoa nyumba au duka la mtu na kuchukua samani za ndani, pesa au bidhaa nyingine yoyote.

Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa kipolisi Tarime/Rorya naibu kamishna Sweetbert Njewike,amekiri kuwepo kwa kikundi hicho ambacho pia kinahusishwa na mauaji ya wakazi wawili wa Nyamongo na kuhaidi kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakaobainika kuhusika na ubomoaji wa nyumba za wananchi kutokana na kujichukulia sheria mkononi.