Shilole afanya pati ya aibu!

 Staa wa Bongo Fleva, Zuwena Mohamed ‘Shilole’ akicheza sebene.

AMA kweli mapenzi yana sarakasi! Ndiyo kauli inayoweza kukuponyoka kufuatia tukio la staa anayebeba dhamana mbili katika sanaa ya Bongo, akitambulika kwenye uigizaji na Bongo Fleva, Zuwena Mohamed ‘Shilole’, ambaye ameangusha bonge la pati ya aibu iliyojaa minong’ono kuwa ni sehemu ya furaha yake isiyo kifani ya kuachana na aliyekuwa mwandani wake, Naftal Mlawa ‘Nuh Mziwanda’, Amani lina kila kitu.

TUJIUNGE NYUMBANI KWA SHILOLE
Tukio hilo la aina yake lililohudhuriwa na baadhi ya mastaa Bongo, lilijiri usiku wa kuamkia juzi (Jumanne) nyumbani kwa staa huyo, Kijitonyama jijini Dar ambapo mwanadada huyo aliandaa shughuli hiyo kwa kuangusha mbuzi wanne, kuku zaidi ya 50 waliopoteza uhai na vinywaji mbalimbali vyenye thamani ya shilingi milioni 2.8.

Katika pati hiyo, Shilole aliwaalika mastaa wenzake na watu mbalimbali ambao walijitokeza kwa wingi kwa ajili ya kumpa kampani katika kusherekea siku hiyo na kujipongeza naye kwa pamoja.

 Baadhi ya mastaa waliokuwepo kwenye hafla hiyo.

SHISHI AFUNGUKA
Akizungumza na gazeti hili kwenye sherehe hiyo, Shilole au Shishi Baby alifunguka kuwa amekuwa akitaabika mno kwenye maisha yake ya kimapenzi alipokuwa na jamaa huyo hivyo kwa sasa hana budi kujipongeza kwa kutua mzigo mzito ambao ulikuwa ukizorotesha maendeleo ya maisha yake tangu amejiingiza kwenye penzi la Nuh ambaye alimtaja kama Marioo (mwanaume anayemtegemea mwanamke kiuchumi).

Shishi alidai kuwa kwa sasa ametua mzigo mzito uliomwelemea kwani alikuwa akilazimika kumhudumia kama mmoja wa watoto wake.

MSIKIE SHISHI
“Jamani acheni tu nijipongeze kwa hili maana sijawahi kuwa na mzigo mzito kama huu maishani mwangu, namshukuru sana Mungu kwa kuniwezesha kuchukua uamuzi huu wa kutengana na Nuh kwani ni mtu ambaye alikuwa mzigo mkubwa sana kwangu kwani ilifikia wakati naishi ndani hata shilingi kumi ya balance nakosa.

 Linah akikata mauno.

“Nimechoka kumhudumia kila kitu kama mtoto, lakini pamoja na kumfanyia hayo hakuwa na shukrani, utadhani alikuwa ameniteka na nguvu za giza.

“Namshukuru sana Mungu kwani tangu nimeamua kuchukua hamsini zangu mambo yangu yananiendea vizuri, yaani sijawahi kukwama kwa lolote, acha nijipongeze na familia yangu maana nilisemwa sana juu ya huyu kijana ambaye hana nyuma wala mbele.

“Sitarajii tena kujiingiza kwenye mapenzi ya kizembe kama haya niliyokuwa nayo mwanzo zaidi sasa nafikiria kujikita kwenye shughuli zangu na kuendeleza familia yangu kwa ujumla, mambo ya mwanaume mpya siyatarajii kabisa kwani nimetosheka,” alisema Shilole.

LINAH ASAULA KWEUPE
Katika shughuli hiyo, ukiachilia mbali vinywaji na mambo mbalimbali yaliyojitokeza, baadhi ya vioja vilivyotawala hisia za waalikwa wengine ilikuwa ni pamoja na kucheza muziki kwa Estelina Sanga ‘Linah’ ambaye alijikuta akisaula nguo kweupe na kuacha sehemu kubwa ya mwili wake ikiwa wazi hivyo kuifanya pati hiyo kuwa ya aibu kufuatia baadhi ya mastaa wakilewa na kufanya mambo ya chumbani hadharani.

KAJALA, CHEGGE VERY CLOSE
Kwa upande wake, staa wa filamu za Kibongo, Kajala Masanja, muda mwingi alionekana kuwa very close (karibu sana) na mkali wa Bongo Fleva, Said Juma ‘Chegge Chigunda’ au ‘Mtoto wa Mama Said’ hadi muda wao wa kuondoka ambapo walitokomea kusikojulikana hivyo kuibua sintofahamu.

NUH ANASEMAJE?
Kuhusiana na tuhuma zilizoshushwa kwa Nuh, gazeti hili lilimtafuta jamaa huyo lakini juhudi za kumpata ziligonga mwamba kufuatia simu yake ya kiganjani kutokuwa hewani kila alipotafutwa.