Wawindaji haramu 3 wakamatwa Maswa

 Polisi nchini Tanzania wanasema kuwa wamewakamata washukiwa watatu wa mauaji ya rubani mmoja Muingereza aliyekuwa akisadia kupepeleza visa vya mauaji ya ndovu katika mbuga ya wanyama ya Maswa.

Rubani huyo Roger Gower aliaga dunia baada ya wawindaji haramu kumfyatulia risasi .
Msemaji wa shirika linalosimamia mbuga za wanyama nchini Tanzania Pascal Shelutete amesema kuwa mizoga tatu ya ndovu ilipatikana karibu na eneo la ajali dhihirisho kuwa aliyeishambulia helikopta hiyo alikuwa amejihami vilivyo na huenda alikuwa na shehena hiyo ya meno ya ndovu.

Msako bado unaendelea Kaskazini mwa Tanzania, kulitafuta kundi la majangili wanaouwa tembo, na ambalo lilimpiga risasi na kumuuwa rubani huyo kutoka Uingereza.

Roger Gower aliweza kutua ndege yake katika mbuga ya Maswa, baada ya kupigwa risasi na kujeruhiwa, lakini alikufa baadae kutokana na majaraha aliyopata.

Mbunge mmoja wa Tanzania, Lazaro Nyalandu, alilaani mauaji hayo na kusema kuwa ni waovu na waoga.

Shirika moja la wakfu wa utunzaji wa mazingira, ndilo lililotangaza kuwa rubani mmoja raia wa Uingereza, alikuwa amepigwa risasi na kuuawa kaskazini mwa Tanzania.

Rubani huyo inasemekana alikuwa akipepeleza mzoga wa ndovu porini alipodunguliwa na mwindaji haramu aliyekuwa amejificha .

Operesheni hiyo ilikuwa katika mbuga ya wanyama pori ya Maswa Kaskazini mwa Tanzania.
Shirika hilo lenye makao yake nchini Marekani- The Friedkin Conservation Fund, linasema kuwa rubani Roger Gower, alikuwa akiwasaidia utawala nchini Tanzania kukabiliana na wawindaji haramu katika maeneo ya Serengeti, aliposhambulia .

Familia ya marehemu inatarajiwa nchini Tanzania hii leo kuandaa mipango ya maziko.
Hivi karibuni, utawala nchini Tanzania umekuwa ukikosolewa kwa kushindwa kutoa maelezo ya kina kuhusiana na uwindaji haramu wa pembe za ndovu.

Uwindaji haramu umeenea sana katika pori ya Maswa na sio tukio la kwanza ambapo wanaharakati wanaolinda wanyama wa porini wanashambuliwa na wawindaji haramu.