Zaidi ya watu 250 wanapata ulemavu kila mwaka nchini kutokana na kuugua ugonjwa wa Ukoma

Zaidi ya watu 250 wanapata ulemavu wa kudumu kila mwaka nchini kutokana na kuugua ugonjwa wa ukoma hali inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na waathirika kutengwa na kunyanyapaliwa na jamii licha ya maradhi hayo kutibika endapo mtu atakayegundulika kuwa nayo atawahi kupata matibabu mapema.

Hayo yamebainishwa na waziri wa afya maendeleo ya jamii jinsia watoto na wazee Ummy Mwalimu wakati akitoa tamko la wizara kuhusu maadhimisho ya siku ya ukoma duniani ambapo amesema kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa mwaka 2014 jumla ya watu 2134 nchini waligundulika kuwa na maradhi hayo huku 271 kati yao ambao ni sawa na asilimia 13 wakipata ulemavu wa kudumu kutokana na kukatika kwa baadhi ya viungo vyao.

Beatrice Mutayoba ni meneja wa mpango wa kudhibiti kifua kikuu na ukoma kutoka wizarani ambapo anasema ugonjwa wa ukoma bado upo kwenye halmashauri 17 nchini mbili kati ya hizo zikiwa Tanzania Zanzibar huku mikoa ya Lindi na Mtwara ikiongoza na historia inaonyesha tangu kugundulika kwa maradhi ni maeneo hayo tu ndio yamekuwa yakiripotiwa kuwepo kwa maambukizi ya juu bila kuwepo kwa sababu za kitaalamu.

Kwa upande wake Dk Deus Kamara mratibu wa kudhibiti ukoma na kifua kikuu akizungumzia kuwepo kwa makambi ya wagonjwa wa ukoma ambayo yanadaiwa kutelekezwa na serikali amesema tayari makambi hayo yalishafungwa zaidi ya miaka 10 iliyopita lakini watu waliokuwa wakiishi kwenye makambi hayo wameendelea kuishi kutokana na jamii kuwatenga hivyo hawana mahala pa kwenda.

Tanzania ni miongoni mwa nchi 17 duniani ambazo bado zina maambukizi ya ugonjwa wa ukoma ambao waathirika wake wanashindwa kushiriki katika shughuli mbalimbali ikiwemo za kiuchumi na kusababisha hasara kwa familia na taifa kwa ujumla.