Auawa Kwa Kuchomwa Kisu Akigombea Mwanamke Baa


Watu  wawili wameuawa mkoani Shinyanga katika matukio mawili tofauti, likiwamo la kijana kuchomwa kisu akigombea mwanamke katika baa ya Matunu mjini Shinyanga.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Dismas Kisusi alisema tukio la kwanza ni la juzi saa 6:00 usiku katika eneo la baa hiyo iliyopo mtaa wa Kaunda, kata ya Shinyanga Mjini, ambapo mwendesha bodaboda aliuawa kwa kuchomwa kisu akigombea mwanamke.

Kisusi alimtaja aliyeuawa kuwa ni Jumanne Ramadhani (22) mkazi wa Ndala katika Manispaa ya Shinyanga, ambaye alichomwa kisu kifuani upande wa kushoto na Emmanuel Shombe (20) mkazi wa Majengo na mfanyakazi wa kampuni ya Mobisolar inayojihusisha na uuzaji wa umeme wa jua.

Akielezea zaidi kuhusu tukio hilo, Kaimu Kamanda Kisusi alisema chanzo cha tukio hilo ni Ramadhani kutaka kumchukua kwa nguvu dada wa Shombe, Ester Shombe (18) mkazi wa Majengo mjini hapa.

“Ramadhani alikuwa analazimisha kumchukua kwa nguvu Ester ndipo kaka yake aitwaye Emmanuel akachukua kisu na kumchoma nacho kifuani upande wa kushoto kulikomsababishia kuvuja damu nyingi, alifariki akiwa njiani kupelekwa hospitali”, alieleza Kisusi.

Alisema Polisi inawashikilia watu wanne kwa ajili ya mahojiano zaidi kuhusu tukio. Wanaoshikiliwa ni Shombe, Ester, Joseph Amos na Tausi Mathias.

Katika tukio la pili, mlinzi na mkazi wa kijiji cha Isaka Station, wilayani Kahama, Moshi Saliboko (36) ameuawa kwa kunyongwa huku miguu yake ikiwa imefungwa kamba umbali wa mita 15 kutoka lindoni kwake katika ofisi za kampuni ya simu ya Zantel. Kisusi alisema Saliboko aligundulika kuuawa juzi saa 1:00 asubuhi katika kitongoji cha Majengo, kijijini humo.

Alisema Saliboko aliuawa kwa kunyongwa huku miguu yake ikiwa imefungwa kamba kisha wauaji kupora vipande vinne vya betri, rada aina ya 165AH, betri 1PG na transfoma (3CUWENT). Alisema baada ya tukio wauaji walitokomea kusikojulikana.