Mwanamke mbaroni kwa kukutwa na meno ya tembo Moro

Jeshi la polisi mkoani Morogoro linamshikilia mwanamke mmoja Magreth Mosha mkazi wa Kibaha mkoani Pwani kwa tuhuma ya kupatikana na vipande saba vya meno ya tembo.

Jeshi hilo pia linamshikilia Bw. Hamis Balewa mkazi wa kijiji cha Mbasa wilayani Malinyi kwa kukutwa na nyama ya sheshe kilo ishirini zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni moja.

Akizungumzia tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Morogoro SACP Urich Matei amesema watu hao walikamatwa katika matukio mawili tofauti ambapo tukio la kwanza limetokea katika nyumba moja ya kulala wageni iliyopo katika manispaa ya Morogoro ambapo akiwa na vipande saba vya meno ya tembo.

Katika hatua nyingine watu watano wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoani humo katika matukio tofauti wakiwemo watumishi watatu wa shirika la ugavi wa umeme Tanzania (TANESCO) mkoani humo baada ya mfanyakazi mwenzao Deo Elias kufariki dunia baada ya kunaswa na umeme wakati akiwa kazini .

Akizungumzia matukio hayo kamanda wa polisi Urich Matei amesema katika tukio la kwanza watu wawili wakazi wa jijini Dar-es-salaam bw. Arisha Shaaban na Bi Zainabu Athuman wanashikiliwa kwa kukutwa na debe sita za bangi huku wafanyakazi watatu wa shirika la TANESCO Bw Ramadhani Yusuf, Bi Elizabeth Kihimbo na Bw Jonas Sajinga wakishikiliwa kuhusiana na kifo cha mtumishi mwenzao.

Watuhumiwa wote wanaohusika na matukio hayo wanatarajia kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili mara baada ya upelelezi wa jeshi hilo kukamilika.