MR. BLUE: SUGU AMEHATARISHA NDOA YANGU

MKALI wa Muziki wa Hip Hop, Bongo Kheri Sameer ‘Mr Blue’ ameendelea kumporomoshea lawama Mbunge wa Mbeya Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambaye pia ni msanii wa Muziki wa Hip Hop, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ kuwa usumbufu aliokuwa anampa ili kuiachia ngoma yake ya Freedom ulimsababishia ‘rabsha’ ndani ya ndoa yake.

Shutuma hizo anazozitoa Blue ni mwendelezo wa ‘drama’ inayoendelea kati yake na Sugu ambayo kwa sasa ndiyo habari ya mjini kufuatia madai ya Blue kuwa mheshimiwa huyo alimzunguka kwa kuuchukua wimbo wake huo ambao mwanzo yeye alimshirikisha, akaurekodi upya huku akifuta mashairi yake lakini kama haitoshi ‘akashuti’ video, jambo ambalo Blue analiona kuwa ni uonevu.

“Kwanza Sugu alinisababishia matatizo ndani ya ndoa yangu mpaka nikawa sipokei simu zake. Alikuwa ananipigia simu kila muda na kila siku akiuliza ‘project’ inatoka lini hadi mke wangu akawa anauliza kuna nini kati yetu.

 Mwanzoni nilimweleza hali halisi lakini kwa namna Sugu alivyokuwa ananisumbua ilifika hatua mke wangu akadhani kuna jambo lingine tofauti, kukawepo na rabsha za hapa na pale lakini sasa nimeweka mambo sawa,” alisema Blue.

Alipotafutwa Sugu kuhusu suala hilo, hakupokea simu na hata alipotumiwa ujumbe mfupi, hakujibu lolote.