Yanga kujinoa dhidi ya Waghana

Klabu ya soka ya Yanga inatarajia kuanza mazoezi ndani ya siku mbili kwa ajili ya mechi dhidi ya klabu ya Medeama ya Ghana na kambi itakuwa kati ya Dar es Salaam au Mwanza.

Meneja wa klabu hiyo, Hafidh Saleh amesema wachezaji wamepewa mapumziko ya siku mbili tu.

Yanga inatarajia kuivaa klabu ya Medeama kutoka Ghana katika mechi itakayopigwa Julai 15 kuwania Kombe la Shirikisho barani Afrika.

Yanga inalazimika kufanya juu chini kuifunga Medeama ili kuamsha matumaini angalau ya kusonga nusu fainali.

Ugumu unatokana na vipigo mara mbili, ikianza kufungwa kwa bao 1-0 ikiwa ugenini dhidi ya Mo Bejaia ya Algeria, halafu ikapigwa tena moja lingine ikiwa nyumbani dhidi ya TP Mazembe.