MAYAI YASIPOIVA NI HATARI

Mayai ni moja ya vyakula vyenye viini lishe muhimu kwa ajili ya afya ya mwili wa binadamu. Kwa kawaida mayai kabla ya kuliwa, huandaliwa kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuchemshwa, kukaangwa au kuchanganywa na vyakula vingine kama vipande vya viazi mviringo ambavyo ni maarufu kwa jina la chips.

Pia, kuna baadhi ya watu wanaopendelea kula mayai mabichi kama dawa ya tiba mbadala, kwa ajili ya kulainisha sauti na wengine hupendelea kula mayai ya kukaanga ambayo hayakukaushwa vizuri.
Ukitembelea migahawa mingi utabaini kuwa watu wanakuwa na mitazamo tofauti na wanavyopenda kula mayai.

Mfano kuna wanaoagiza watengenezewe mayai kwa mtindo unaojulikana kama ‘macho ya ng’ombe.’ Ukiagiza namna hiyo, mpishi atataka kuuliza kama ni ‘macho ya ng’ombe’ ya kugeuza.

Ina maana kuwa ‘macho ya ngombe’ ya kugeuzwa ni yale yanayoivishwa pande zote lakini yale ambayo siyo ya kugeuza, huwa linaiva nusu. Upande mmoja unabaki ukiwa mbichi, na ndiyo raha ya baadhi ya watu.

Hata ukienda kwa wakaanga chipsi, utakuta wanawauliza wateja wao kama wanapokaanga na mayai wakaushe au wasikaushe. Hii inaashiria kuna watu wanataka wale chipsi zikiwa na mayai ambayo halijaiva sawasawa.

Kuna watu wengine wanaamini kwamba kula mayai mabichi kunafanya sauti inakuwa nyororo, hivyo wale waimbaji huwalazimu kufanya hivyo ili kufanya nyimbo zao zivutie.

Si hivyo tu, kuna baadhi ya watu huamini pia dawa ya kikohozi ni kunywa yai bichi lililochanganywa na asali. Hizi ni imani ambazo zimejengeka kwenye jamii na watu hufanya hivyo ili kufikia malengo waliyokusudia.

Katika siku za karibuni, imevuma kuwa mayai ya kwale yanatibu magonjwa sugu kama vile kisukari, shinikizo la damu, saratani na kifua.

Katika mpango huo, wanapendekeza wahusika kula mayai mabichi ya kwale tena kwa kutafuna hadi kaka lake, yaani ganda la nje.

Hali hii imesababisha biashara ya mayai ya kwale kuwa kubwa na hata wafugaji wameongezeka mara dufu.