Chris Brown Akamatwa kwa Kumtishia Mauaji Mwanamke

Los Angeles
Polisi wa Los Angeles nchini Marekani wamemkamata na kumshikilia mwanamuziki marufu wa R&B, Chris Brown kwa tuhuma za kushambulia mtu kwa silaha hatari.

Polisi waliitwa kwenye makazi ya Chris Brown na mwanamke aliyeomba msaada kwao ikiwa majira ya saa 9 usiku wa kuamkia jana. Malkia wa urembo, Baylee Curran ameambia Gazeti la LA Times, kwamba mwanamuziki huyo alimwelekezea mtutu wa bunduki.

Hata hivyo walizuiwa kuingia na ilibidi wasubiri hadi kupata idhini ya jaji kabla kufanya msako wa kutafuta bunduki katika makaazi hayo.

Mwanamke huyo aliyewaita polisi baadaye aliambia vyombo vya habari kwamba walitofautiana na Brown kuhusu majohari.

Alisema alikuwa ameingia kwa Bw Brown akiwa na rafiki yake na mshirika wa kibiashara na alikuwa akiangalia mkufu wa thamani uliokuwa umevaliwa na mwanamume mmoja pale mwanamuziki huyo alipomkaripia na kumtaka aondoke mara moja akiwa amemwelekezea bunduki.
Alifanikiwa kuondoka makazi hayo bila madhara. Chris Brown ameandika ujumbe kwenye mitandao ya kijamii kujitetea na kuwalaumu polisi kwa kumhangaisha.

Wakili wake alifika kwenye makaazi hayo na kumsihi aandamane na maafisa wa polisi. Mwanamziki huyo anatarajiwa kufunguliwa mashtaka ya uvamizi.

Chris Brown amewahi kujipata matatani awali, hususan alipomshambulia aliyekuwa mpenzi wake na mwanamziki Rihanna hapo Februari 2009.