Hali ya biashara nchini siyo nzuri - JWT

Hali ya biashara maeneo mbalimbali nchini hivi sasa sio nzuri, kutokana na idadi kubwa ya watanzania kukosa uwezo na nguvu ya kipesa ya kufanya manunuzi.

Tatizo hilo linalodaiwa kuchangiwa na sababu kadhaa mojawapo ikiwa ni kiwango kikubwa cha kodi ya forodha kinachotozwa kwa bidhaa zinazoingizwa nchini.

Mkurugenzi wa Idara ya Habari wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, (JWT), Bw. Stephen Chamle, amesema hayo leo na kuongeza kwamba hali imekuwa mbaya kiasi cha baadhi ya wafanyabiashara kulazimika kuagiza bidhaa kutoka nchi za jirani kama njia ya kutafuta unafuu wa kodi, tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo Tanzania ndiyo ilikuwa soko la bidhaa kwa nchi za jirani kama Kenya, Uganda, Rwanda na Zambia.

Aidha, Bw. Chamle amesema wao kama jumuiya wanaunga mkono zoezi linaloendelea sasa la uhakiki wa namba za utambulisho wa mlipakodi maarufu kama TIN, kwa maelezo kuwa zoezi hilo litasaidia kupunguza kichaka cha ukwepaji kodi kilichokuwa kinafanyika kupitia matumizi yasiyo sahihi ya namba hizo.