F Jinsi ya Kupunguza Unene | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

Jinsi ya Kupunguza Unene

Watu wengi sana wanatafuta njia za kuweza kupunguza uzito wa miili yao au kwa maneno mengine, watu wengi wanene hutumia njia mbalimbali ili wawe wembamba. Kutokana na hilo, watu wengi wanajitokeza na kujipatia fedha kwa kudai kuwasaidia watu hao katika kupunguza uzito wa miili yao.

Kwetu hapa Tanzania, njia zinazotumika ni dawa za asili (hapa namaanisha dawa zilizotengenezwa hapa hapa kienyeji au mitishamba) na dawa zilizoletwa na makampuni mbalimbali ya nje ya nchi, zikiwemo za asili na za kemikali. Kila mmoja aliyetumia dawa hizo amekuwa na maoni tofauti, wapo walioridhika na matokeo na wapo ambao waliona dawa hizo hazikuwafaa.

Katika kutumia dawa hizo yapo mambo ambayo yanapaswa kutazamwa, si tu kupungua au kutopungua uzito bali na matokeo mengine ambayo yanasababishwa na matumizi ya dawa hizo (side effects). Najua hakuna aliyechukua hatua ya kufanya utafiti huo, lakini kitu cho chote unachotumia huwa na matokeo mengine mengi ambayo hayakuwa yamekusudiwa.

Tatizo la kupunguza uzito si la hapa kwetu tu, ni la ulimwengu mzima. Sasa jee, wenzetu wenye utaalamu zaidi wanasemaje kuhusu hili?


Njia Sahihi Za Kupunguza Uzito
Pamoja na kwamba kuna mambo mengi yanayotajwa na kutumika kama njia za kupunguza uzito, kiutaalamu yote yanalenga kupunguza mafuta (fat) mwilini. Hivyo basi njia sahihi za kupunguza uzito huo ni mbili. Ya kwanza ni kuwa na mpango maalumu kuhusu chakula na namna unavyokula na ya pili ni kufanya mazoezi ili kupunguza mafuta yaliyojazana chini ya ngozi (adipose tissues). Katika kufanya hayo yote, inabidi kuwa na malengo katika kupunguza uzito wako. Kuna kiwango cha chini cha uzito ambacho kila mtu inafaa awe nacho kulingana na umri na urefu alio nao. Kupunguza uzito chini ya kiwango hicho kunaweza kuleta matatizo mengine ya afya baadaye. Inafaa basi kabla ya yote kujua unataka kupunguza uzito kwa kiasi gani. Sasa tutazame kila moja ya njia hizo hapo juu za kupunguza uzito.

Mpango Wa Chakula Na Namna Ya Kula
Kusudi mwili uwe na nguvu, kila wakati unahitaji kuvunjavunja na kuunguza mafuta yaliyomo mwilini. Endapo mwili utagundua hakuna chakula tumboni, utaacha kuunguza mafuta na badala yake utaanza kuvunjavunja misuli ya mwili. Imethibitishwa kwamba watu wanaokula milo mitatu kwa siku wanapunguza uzito wao zaidi ya wale wanaopata milo pungufu. Hii ina maana gani? Maana yake ni kwamba siyo sahihi kufikiri kuwa unaweza kupunguza uzito kwa kupunguza kula.

Kupunguza uzito kwa njia inayofaa ni kula milo ya kawaida na chakula cha aina fulani na kamwe si kwa kuruka milo.

Chakula Cha Kupunguza Uzito
Kusudi kupunguza uzito mwili unahitaji milo iliyokamilika. Milo hiyo iwe na chakula cha makundi yote yaani protini (protein), wanga (carbohydrates) na matunda. Kitu cha kuzingatia ni uwiano wa chakula hicho katika mlo mmoja. Kufanya yafuatayo kutasaidia kupunguza uzito wa mwili wako:


  1. Kula chakula chenye kalori ndogo kwa wingi. Hapa ina maana inakupasa kula matunda na mboga kwa wingi zaidi ili kulifanya tumbo lako lijae. Waweza kutengeneza mlo wako ukawa hadi asilimia 50% kuwa ni mbogamboga tu.
  2. Tumia zaidi nafaka nzima kuliko chakula cha wanga kilichosagwa
  3. Tumia mafuta kidogo ya kupikia
  4. Jenga tabia ya kula nyumbani na si hotelini. Kula hotelini kunasababisha ule zaidi ya kipimo na kuna tatizo jingile la kutokujua chakula hicho kiliandaliwa kwa kutumia viungo gani na kwa vipimo vipi.
  5. Kunywa maji mara nyingi kwa siku. Kwa mwanamme kunywa maji hadi lita 3 kwa siku na mwanamke lita 2 kwa siku. Maji yana faida nyingi sana mwilini lakini pia hujaza sehemu fulani ya tumbo na kitu kisicho na kalori kabisa. Maji baridi yanafaa zaidi kusudi mwili utumie kalori kuyapasha hadi kufikia joto la mwili. Ukijijengea tabia ya kunywa maji nusu lita, nusu saa kabla ya kula chakula itakusaidia sana hasa kama una umri mkubwa.


Mazoezi Ili Kuunguza Kalori
Jiwekee mpango wako mzuri wa kufanya mazoezi. Ikiwa ulikuwa hufanyi mazoezi kabisa, anza taratibu kwa mazoezi ya nusu saa, mara tatu kwa wiki na kuongeza muda taratibu. Unaweza kuanza kwa kuzunguka hapo nyumbani tu kwanza.

Ukiweza kwenda kufanya mazoezi gym chini ya watu waliofunzwa itakuwa bora zaidi. Mazoezi mengine unayoweza kufanya ni kama yoga, karate, kickboxing n.k. Unaweza kujiunga na michezo kama mpira wa miguu, volleyball, tennis, haya yote yatakusaidia zaidi.

Mazoezi Ya Kupunguza Mwili Na Tumbo
Hapa chini nitaonyesha video mbili ambazo zitaweza kukusaidia kufanya mazoezi ya kupunguza mwili.  Angalia video hizo kisha changua moja ya kuanza nayo, hakikisha unajiwekea mpango mzuri wa kufanya mazoezi haya. Video ya kwanza ni ya dakika kama 8 yenye lengo la kupunguza vyote, mwili na mafuta ya tumbo. Bonyeza juu ya picha hii hapa chini kuangalia video hiyo:

Video ya pili ni fupi zaidi, kama dakika tano tu na inalenga zaidi katika kuunguza mafuta ya tumbo. Angalia video hiyo kwa kubonyeza juu ya picha hii hapa chini: