Kanumba hajaondoka na tasnia japo imeshuka - JB

 Muigizaji na muongozaji wa filamu nchini Tanzania, Jacob Stephen maarufu kama JB amesema kushuka kwa filamu za nchini (Bongo Movie) hakuhusishwi na kifo cha aliyekuwa muigizaji nguli marehemu Steven Kanumba.

Alipofanyiwa mahojiano na eNewz, JB amekiri kuwa tasnia ya filamu nchini imeshuka kiwango lakini akakazia kuwa kushuka huko ni kwa msimu pekee.

“Ni kweli tasnia ya Bongo movie kwa sasa imefifia ila naamini ni msimu tu kama ilivyotekea kwenye bongo fleva kipindi cha nyuma ilipotea lakini kwa sasa imerudi na ipo juu kwahiyo hata kwa Bongo Movie itarudi tu juu naamini ni wakati tu haujafika” amesema Jacob Stephen.

Hata hivyo JB amezidi kupingana na mawazo ya watanzania wengi kuwa marehemu Steven Kanumba ameondoka na tasnia ya filamu nchini.

Jacob Stephen amesema “Watu wanadhani kwamba Kanumba alikufa na bongo movie sio kweli japo inafahamika wazi kwamba Kanumba alikuwa muigizaji mzuri lakini kuna waigizaji wengine kama kina Ray, Riyama na wengine ambao ni wazuri na bado wapo”.