Tanzania yanufaika na miradi ya ICF

Tanzania ni moja ya nchi zilizonufaika na uwezeshaji ambao umekuwa ukitekelezwa na taasisi inayojishughulisha na uboreshaji wa mazingira ya uwekezaji barani Afrika ya Investment Climate Facility – ICF.

Moja ya malengo ya taasisi hiyo imeelezwa kuwa ni kuona nchi za Afrika zinasimamia zednye mipango ya kukuza uchumi na uwekezaji.

Mwenyekiti Mwenza wa Taasisi hiyo, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mzee Benjamin William Mkapa, amesema hayo katika mkutano na wanahabari jijini Dar es Salaam hii leo, mkutano ambao lengo lake ni kutoa ripoti ya mafanikio yaliyopatikana na ICF tangu kuanzishwa kwake mwaka 2007.

Rais Mstaafu Mkapa ametaja baadhi ya maeneo ambayo Tanzania imenufaika kutokana na kuwa nchi mwanachama wa ICF kuwa ni maboresho katika usajili wa biashara, uwazi na ufanisi katika mfumo wa forodha, maboresho katika sheria na taratibu za kodi pamoja na mfumo bora wa kisheria wa utatuzi wa migogoro ya kibiashara ambayo kwa ujumla wake imesaidia kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi.