Vijana wanaotengeza runinga kutoka kwa kompyuta Rwanda

 Nchini Rwanda vijana wanazidi kukuna vichwa kubuni miradi ya kujiendeleza wakati huu ambapo wanakabiliwa na ukosefu wa kazi.

Vijana katika mji wa Ruhango kusini mwa nchi hiyo walijiweka pamoja na kubuni mradi wa kutengeneza runinga kutoka kwa komputa zilizozeeka au ambazo ziliharibika.Runinga hizo zinapatikana kwa bei nafuu kuliko zile zinazotengenezwa ng'ambo.

Mwandishi wa BBC Yve Buchiana alitembelea mojawapo ya karakana ndogo kunakokusanywa mashine za kompyuta zilizoharibika tayari kwa kutengenezwa na kugeuzwa kuwa runinga.
Ni katika karakana hiyo ambapo aliweza kukutana na Uwamahoro Charlotte ambaye alipata mafunzo yake ya kiufundi kwenye shule hii kabla ya kuwa mwalimu:
''Hii kama mnavyoiona hapa ni kompyuta.Nyingi hutupwa kwa kuharibika au tu kwa kuwa sokoni kumeletwa aina mpya.Nilipofika hapa walinifundisha namna ya kubadilisha hizo komputa na kuzifanya ziwe runinga.Ndivyo ninavyofundisha watoto hawa.

Kuna kipande kidogo ambacho ni kama bamba.Kiufundi kuna namna tulivyojifunza ya kuunganisha mitambo ya komputa ya kawaida na hilii bamba la runinga.na mambo kwisha''.

 Kwenye masoko,runinga zilizotengenezwa kutoka komputa zimeanza kushinda na nyingine kutoka ng'ambo,hali inayowafanya wabunifu wa mradi huu kuanza kujipiga kifua.Alphonse Bimenyimana ni mkuu wa mradi huu:
''Unavyojua ni kwamba kwa sasa kwenye maduka mengi zinapatikana tu runinga za flat Screen ambazo bei yake si kila mwananchi anayeweza kuimudu.

Sisi tuliona kwamba hizi runinga ndogo za kawaida zinatoweka sokoni .Hizi zetu tunazotengeneza bei yake iko chini sana ,ndiyo maana tumeanza kupata ofa kutoka kwa watu mbali mbali wakiwemo pia wafanyabiashara''

Mwandishi huyu aliingia katika maduka yanayouza bidhaa zao na kukutana na baadhi ya wauzaji
''Mimi nauza runinga hapa .Wateja wanakuja kwa wingi kutafuta hizi za HP zinazotengenezwa kutoka kwa komputa ambazo bei yake ni franga elfu 45 za Rwanda.Wengi hununua hizi HP kwa sababu ziko kwa bei wanayomudu''
Wanaosomea katika shule hii , wengi walihitimu shule za sekondari na hata wengine vyuo vikuu,lakini wakakosa ajira.Madukani runinga moja hupatikana kwa dolla 50 za Marekani.