Watanzania Watakiwa kupima afya kuepuka homa ya ini

Dalili za Ugonjwa wa Homa ya INI na Jinsi Unavyoambukizwa.


Watanzania wametakiwa kuwa na mazoea ya kwenda kupima afya zao mara kwa mara pamoja na kuepuka ngono zembe ili kuepuka maambukizi mapya ya homa ya ini ugonjwa ambao tiba yake mpaka sasa bado ni changamoto.

Hayo yamebainishwa leo na Mkurugenzi wa Afya kutoka Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dkt. Goodluck Moshi ambapo amesema kuwa serikali inatakiwa kutoa elimu zaidi kwa wananchi juu ya madhara ya ugonjwa huo pamoja na kujikinga na maambukizi mapya ya ugonjwa huo.

Dkt. Moshi amesema kuwa taifa sasa linatakiwa kujipanga kuanzia mashule na kuweka mtaala maalum unaoelezea homa ya Ini lakini pia vyombo vya habari pamoja na mahospitali kwa kufanya hivyo nchi inaweza kuzuia kwa kiasi kikubwa kuenea kwa ugonjwa huo.

Aidha amesema kuwa serikali inatakiwa kusisitiza kupata chanjo kuanzia kwa watoto pamoja na watu wazima ingawa upatikanaji wake una gharama za juu lakini haina budi kufanyika jitihada za kupatikana kwa chanjo hiyo ili kujikinga na ugonjwa huo hatari.