Yanga uso kwa uso na Mazembe leo bila nyota wake kadhaa

YANGA SC leo ipo dimbani jijini Lubumbashi, Congo DR kucheza mchezo wao wa kukamilisha ratiba wa kundi A kwenye Kombe la Shirikisho Afrika, watakapovaana na miamba TP Mazembe ambao tayari wana tiketi ya nusu fainali mkononi, mchezo utakaopigwa majira ya saa 9:30 kwa saa za Afrika Mashariki.

Yanga wanaingia kwenye mchezo huo huku wakiwakosa wachezaji wao kadhaa kutokana na kuwa na majeraha na kutumikia adhabu ya kadi za njano.

Watakaoukosa mchezo huo kutokana na majeraha ni nahodha Nadir Haroub, Obrey Chirwa, Juma Abdul na Vincent Bossou wakati Kelvin Yondan na Donald Ngoma wakikosekana kutokana na kutumikia adhabu yao ya kadi ya njano.

Timu nyingine ambazo zinawania kuungania na TP Mazembe kuelekea hatua ya nusu fainali ni Medeama ya Ghana na MO Bejaia ya Algeria, ambazo zinakutana nchini Algeria kusaka nafasi moja iliyobaki.

TP Mazembe wanaongoza wakiwa na alama 10, wakifautiwa na Medeama wenye alama 8, MO Bejaia wanashika nafasi ya tatu kwa alama 5, huku Yanga akiburuza mkia akiwa na alama 4.

Ushindi au sare ya aina yoyote itaivusha Medeama kwenda nusu fainali, huku MO Bejaia ikihitaji walau ushindi wa kuanzia magoli mawili ili kupata nafasi ya kwenda nusu fainali.

Kwa upande wa kundi B, wao wamebakisha mchezo mmoja tu tayari timu zilizofuzu zimeshajulikana. Timu hizo ni FUS de Rabat ya Morocco na Etoile Sportive du Sahel ya Tunisia.

Mechi za leo Kombe la CAF kwa saa za Afrika Mashariki

9.30 pm TP Mazembe – Congo, DR v Yanga – Tanzania

10.30 pm MO Bejaia – Algeria v Medeama – Ghana

4.30 pm FUS de Rabat – Morocco v ES Sahel – Tunisia

KeshoAgosti 24

4.30 KAC Marrakech (Morocco) v Al-Ahli Tripoli (Libya)

Ratiba ya mechi za nusu fainali

Mechi za kwanza zitachezwa Septemba 16-18 na marudiano yatakuwa Septemba 23-25
Mshindi wa 2 Kundi B dhidi ya Mshindi Kundi A

Mshindi wa 2 Kundi B dhidi ya Mshindi Kundi A

Fainali

Mchezo wa kwanza utachezwa Oktoba 28-30 na Novemba 4-6 utachezwa wa marudiano.