Klopp: Liverpool wanaweza kutwaa taji Uingereza

Meneja wa Liverpool, Jurgen Klopp amesema bado kuna nafasi ya kuimarika kama kikosi chake kinataka kupigania taji la Ligi Kuu ya Uingereza msimu huu hata baada ya kuanza vyema kampeni yao.

Liverpool ambao mara ya mwisho kutwaa ubingwa wa ligi ilikuwa mwaka 1990, waliicharaza Hull City kwa mabao 5-1 Jumamosi iliyopita na kupaa hadi mpaka nafasi nne katika msimamo, wakiwa nyuma ya vinara Manchester City kwa alama tano.

Liverpool wameshinda mechi ngumu za ugenini dhidi ya Arsenal na Chelsea huku wakiwababua mabingwa Leicester City kwa mabao 4-1 msimu huu.

Mechi pekee waliyopoteza ni ile waliyofungwa na Burnley.

Akihojiwa, Klopp amesema ni kweli kwa sasa wanacheza vizuri lakini bado kuna nafasi ya kuimarika ili waweze kuendeleza wimbi lao la ushindi.