CHADEMA yaukataa muswada wa vyombo vya habari

Chama cha Demokrasia na Maendeleo, CHADEMA kimesema kuwa Muswada wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari unaotarajiwa kuwasilishwa kwenye Mkutano wa Bunge unaoanza Jumanne, Novemba 1, mwaka huu, ni hatari.

Chama hicho katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, kimesema kuwa serikali inapaswa kutoa muda zaidi kwa wadau kuujadili ili kushauri na kuondoa mambo ambayo ni hatarishi katika tasnia ya habari nchini.

"Kutokana na Serikali kuamua kupuuza maoni ya wadau na wananchi kwa ujumla kuhusu kuongeza muda wa kujadili na kuboresha Muswada wa Huduma za Vyombo vya Habari, ambao iwapo utaachwa na kupitishwa kama ulivyo unalenga kutunga sheria hatari zaidi dhidi ya vyombo vya habari, haki ya wananchi ya kupata taarifa na hata uhuru wa kutoa maoni"
Kamati Kuu ya Chama hicho katika kikao chake cha kawaida kilichoketi Oktoba 22-23, Jijini Dar es Salaam, pamoja na masuala mengine, imetuma ujumbe wa baadhi ya wajumbe waandamizi wa Kamati hiyo kwenda mjini Dodoma kukutana na Wabunge wa CHADEMA, ili kujadiliana na kutoa maelekezo ya Chama kuhusu muswada huo.

Katika hatua nyingine, chama hicho kimetangaza majina ya wabunge waliochaguliwa kuingia katika Kamati Kuu ya chama hicho kupitia tiketi ya ubunge wao, katika uchaguzi uliofanyika Jumapili, Oktoba 30, mwaka huu, mjini Dodoma.

Wajumbe waliochaguliwa ni pamoja na 
1. Tundu Antipas Lissu
2. Godblesss Jonathan Lema
3. Joseph Osmund Mbilinyi
4. Ester Amos Bulaya
5. Mariam Salum Msabaha