NAMNA YA KUKABILI HARUFU MBAYA YA MIGUUNI

Ukigundua una tatizo hili, hakikisha unasafisha miguu yako mara kwa mara ukiiacha mikavu muda wote ili kuepusha unyevunyevu.

Miguu kutoa harufu mbaya ni tatizo sugu linalowakabili baadhi ya watu katika jamii, wengi wakiwa wanaume.

Katika nyakati hizi za mvua, tatizo hili linaonekana kuzidi kuwa sugu, hali inayosababisha kuwepo na harufu mbaya hasa kwenye mikusanyiko ya watu kama vile kwenye daladala.

Lakini watu wengi wenye tatizo hili huwa wagumu kukubaliana na hali yao hata kutafuta tiba mahususi inaweza kuwaondolea kero hiyo.

Licha ya kuwepo sababu mbalimbali zinazochangia kutokea hali hiyo, ukweli utabaki kuwa uchafu ndiyo chanzo kikuu cha miguu kutoa harufu.

Kwa kiasi kikubwa uchafu huo ndio unasababisha kuzaliwa kwa vijidudu vinavyoleta harufu mbaya kwenye miguu na kuwakera wanaokumbana na harufu hiyo.

Pamoja na tiba nyingine za kitaalamu ambazo mtu mwenye tatizo hili anaweza kupata, usafi ni jambo kubwa analopaswa kuzingatia zaidi hasa kipindi hiki cha mvua.

Ukigundua una tatizo hili, hakikisha unasafisha miguu yako mara kwa mara ukiiacha mikavu muda wote ili kuepusha unyevunyevu.

Kila unapovaa viatu vya kufunika, hakikisha unavaa soksi safi na kavu. Epuka kurudia soksi au kuvaa ambazo hazijakauka vyema kwani zinaweza kusababisha miguu kunuka mara dufu.

Usivae viatu vilivyoloa na endapo ikatokea umenyeshewa, hakikisha unavianika kwenye hewa ili vikauke kupunguza uwezekano wa kutokea harufu.

Kama utahisi tatizo ni kubwa zaidi ni vyema utumie sabuni zenye dawa za kuua vijidudu pamoja na mafuta maalumu yanayoweza kutumika miguuni. Ikishindikana, nenda kwa wataalamu wa afya.