Raia wa Cape Verde ‘Zungu la unga’ kizimbani

LILIANA Jesus (32), mwanamke raia wa Cape Verde aliyekamatwa wiki hii akiwa na dawa za kulevya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (JKNIA), amefikishwa mahakamani leo, anaandika Faki Sosi.

Hellen Mushi, Wakili wa Serikali mbele ya Victoria Nongwa, Hakimu Mkazi katika Mahakama ya Kisutu, amemsomea mtuhumiwa huyo shitaka la kukutwa na dawa za kulevya aina ya Cocaine.
Mushi amedai kuwa Liliana alikamatwa JKNIA, Ilala jijini Dar es Salaam tarehe 18 Oktoba, mwaka huu akiwa na kilogramu 2.380 za dawa hizo za kulevya aina ya Cocaine.

Hata hivyo, wakili Hellen ameiambia mahakama hiyo kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Mtuhumiwa huyo ameshindwa kujitetea mahakamani hapo kutokana na kutojua lugha ya Kiengereza wala Kiswahili ambapo hakimu Nongwa ameamuru arudishwe rumande hadi shauri hilo litakapotajwa tena, mnamo tarehe 3 Desemba, mwaka huu.