Kuumwa Tumbo wakati wa Hethi

KARIBU sana katika makala yetu inayohusu afya.Kutokana na simu nyingi ninazozipata nikiulizwa maswali juu ya maumivu yanayowapata akina mama wengi wakati wa hedhi nimeona ni bora niandike makala hii ili iweze kuwasaidia na wengine kujua nini chanzo na mhusika afanye nini pale anapopatwa na tatizo hilo.

Maumivu wakati wa hedhi (period pains) au kitaalamu dismenorrhea, ni maumivu yanayojitokeza sehemu ya chini ya tumbo au kiunoni wakati mwanamke anapoanza kupata siku zake au kabla ya hapo.

Maumivu hayo huweza kuwa madogo au ya wastani huku baadhi ya wanawake wakipata maumivu makali sana. Maumivu hayo huanza pale yai linapotoka katika mrija (fallopian tube) na kuteremka chini ya mrija huo wakati wa Ovulation.

AINA YA MAUMIVU
Maumivu ya tumbo la hedhi yapo ya aina mbili.  

Ya kwanza ; 
ni maumivu yasiyokuwa na sababu zozote za kimsingi za kitiba. Katika aina hii maumivu ni ya kawaida na huhisiwa sehemu ya chini ya tumbo na kiunoni. Maumivu hayo huanza siku moja au mbili kabla ya hedhi na humalizika baada ya siku mbili au nne.

Aina ya pili ; 
ni yale maumivu yanayojumuisha maumivu yanayosababishwa na sababu nyinginezo za kitiba kama vile matatizo katika kizazi, ugonjwa wa nyonga (PID) na matatizo katika mirija ya mayai.

Nusu ya wasichana na wanawake hupata maumivu wakati wa hedhi na karibu asilimia kumi mpaka kumi na tano  wanasema kuwa hupata maumivu     makali.

Uchunguzi unaonesha kuwa kuna sababu mbalimbali zinazoweza kuongeza uwezekano wa kuumwa tumbo wakati wa hedhi.

Sababu hizo ni kama  kuwa na umri wa chini ya miaka 20, kuvunja ungo wakati wa miaka 11 au chini ya miaka hiyo, kutoka  damu nyingi wakati wa hedhi, wanawake ambao hawajawahi kuzaa.

Magonjwa yanayoweza kusababisha mtu kupatwa na maumivu ya tumbo la hedhi. Miongoni mwa magonjwa hayo ni:

 Endometriosis. 
Hii ni hali ambayo seli za ndani ya mfuko wa uzazi huanza kuoka nje ya fuko hilo, au hata sehemu nyinginezo
Adenomyosis: 
Huu ni ugonjwa wa wanawake ambapo tezi au uvimbe (tumors) zinaota katika mfuko wa uzazi.
PID au Ugonjwa wa uvimbe katika nyonga.
Magonjwa ya zinaa yanayotokana na bakteria au magonjwa ya kuambukiza ya zinaa.
Mlango wa uzazi unapokuwa mdogo kiasi kwamba unazuia damu ya hedhi isitoke kwa urahisi.
baadhi ya magonjwa yanayoweza kusababisha mtu kupatwa na maumivu ya tumbo la hedhi.

Ugonjwa wa uvimbe katika nyonga ambao husababishwa na magonjwa ya zinaa yanayotokana na bakteria au magonjwa ya zinaa.
 dalili za ugonjwa huo ni:
Maumivu kuja na kuondoka, kwa kiwango tofauti (spasmodic).
Maumivu zaidi huwa sehemu ya chini ya tumbo na huchanganyika na maumivu ya sehemu ya chini ya mgongo ambayo husambaa mpaka mapajani.
Kujihisi kutapika, kichefuchefu na wakati mwingine hata kutokwa jasho.
Kupata choo laini au hata kuharisha na wengine hufunga choo.

TUMBO KUWA KUBWA AU KUWA GUMU.
Kupata maumivu ya kichwa, kujisikia kuchoka.
Kiwango cha maumivu ya tumbo la hedhi na mchanganyiko wa dalili inategemea mtu na mtu, mtu mwingine anaweza akawa anapata karibu dalili zote nilizozitaja hapo juu na mwingine ni baadhi tu au hata dalili moja. Wanawake wengi hujitambua  bila hata msaada wa daktari.

USHAURI
Iwapo mwanamke atapata maumivu makali sana ni bora akamuone daktari ili wafanye vipimo kama vile Ultrasound, CT na CT-Scan, MRI na vinginevyo ili kufahamu nini chanzo cha  maumivu hayo kuwa makali

MATIBABU
Matibabu ya maumivu ya tumbo la hedhi kwa kawaida huweza kutibika kwa urahisi kwa kutumia vidonge vya kupunguza maumivu, kama vile 


  • Ibuprofen, 
  • naproxen 
  • au aina nyinginezo za vidonge visivyokuwa na steroids (NSAIDS). 


Pia kuna wakati madaktari wanaweza kumshauri mgonjwa kutumia vidonge vya kuzuia mimba, Vidonge hivyo huzuia mzunguko wa yai au Ovulation na kupunguza ukali wa maumivu ya tumbo la hedhi.

Pia  wanawake wanashauriwa kufanya baadhi ya vitendo ambavyo hupunguza maumivu  hayo, kama 


  1. kuoga maji moto, 
  2. kuweka kitambaa chenye joto katika sehemu ya chini ya tumbo, 
  3. kufanya mazoezi kama yoga, meditation,  
  4. kutumia vidonge vya vitamin E, 
  5. Thiamine na Omega 3
  6.  kumetajwa kuwa husaidia katika suala hilo. 


Wanawake wanaopatwa na matatizo kama hayo ni bora wapumzike vyema na kupata usingizi wa kutosha.

Vilevile unaweza kujiepusha na kupatwa na maumivu ya tumbo la mwezi kwa kufanya yafuatayo:


  1. Kujitahidi kula matunda, 
  2. mbogamboga na kupunguza kula vyakula vyenye mafuta mengi, 
  3. pombe, 
  4. kafeini, 
  5. sodium na sukari, 
  6. kufanya mazoezi ya viungo, 
  7. kujiepusha na wasiwasi na mawazo
  8. kuepuka kuvuta sigara.