Jiji Arusha lasimamisha wafanyakazi 66

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Jiji La Arusha, Athumani Kihamia ametangaza kusitisha mikataba ya wafanyakazi 66 kati ya 132 wasio na kazi za lazima katika halmashauri hiyo.

Amewasimamisha kazi kwa lengo la kubana matumizi ili fedha zitakazookolewa zitaelekezwa kwenye matumizi ya miradi ya maendeleo na ulipaji wa madeni.

Alisema hayo wakati akizungumza na wanahabari ofisini kwake, na kueleza kuwa kabla ya hapo, alikuwa akilipa mishahara ambayo aliibebesha halmashauri mzigo huo mkubwa na kufanya ielemewe na kupoteza fedha ambazo zingetumika kwenye miradi ya maendeleo na ulipaji wa madeni.

Kihamia alisema anasimamia kubana matumizi ili kulipa madeni yenye kero na tija kama ambavyo walielekezwa na Kamati za Bunge na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhakikisha wanabana matumizi yasiyo na ulazima ili kulipa madeni ya muda mrefu.

Akizungumzia tuhuma za ulipaji wa fedha za walimu 701 kiasi cha Sh milioni 169 zikiwa madeni ya walimu ambazo hazikufuata utaratibu wa kuidhinishwa na Baraza la Madiwani au Kamati ya Fedha na Uchumi, alisema fedha hizo zinatokana na mapato ya ndani nasi lazima fedha zinazotumika kuidhinishwa na baraza au kamati ya fedha.