Miili ya wataalamu wawili wa UN waliotoweka yapatikana DRC

Maafisa nchini Jamhuri ya Demokrasi ya Congo wanaamini kuwa wamepata miili ya wafanyakazi wawili wa Umoja wa Mataifa ambao walitoweka nchi humo.

Miili hiyo ilipatikana eneo ambapo raia wa Marekani Michael Sharp na raia wa Sweden Zaida Catalan walitekwa nyara wiki mbili zilizopita.

Miili hiyo ni ya mwanamume na mwanamke ambao wote ni wazungu.

Kumekuwa na ghasia eneo la Kasai, ambapo pia polisi 40 walipatikana wamekatwa vichwa mwishoni mwa wiki.

Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa walikuwa nchini DRC kufuatilia vikwazo vilivyowekwa dhidi DRC, lakini wakati huo walikuwa wakichunguza ripoti za dhuluma eneo la Kasai.

Msemaji wa serikali ya Congo Lambert Mende, alithibitisha ripoti za kupatikana kwa miili hiyo kwa BBC.
Hata hivyo amesema kuwa uchunguzi wa DNA unahitaji kuondoa shaka yoyote kuhusu miili hiyo.

Serikali ya Congo inapigana na kundi la waasi ambalo linahudumu eneo hilo na linaaminiwa kuwateka wataalamu hao.

Ghasia eneo la Kasai zimechochewa kufuatia kuuliwa kwa kiongozi wa kitamaduni Kamuina Nsapu, ambaye alikuwa akiongoza upinzani dhidi ya Rais Joseph Kabila