Lukuvi ataja siri kwenda sawa na kina Mbowe



WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, ameanika sababu za bajeti yake kupitishwa kwa kishindo na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wa upinzani wakiwamo Freman Mbowe ,Halima Mdee na Ester Bulaya wa Chama cha Demnokrasia na Maendeleo (Chadema).


Kuanzia juzi, karibu wabunge wote waliochangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka ujao wa fedha walimpongeza waziri huyo kwa kuchapa kazi na kuunga mkono bajeti ya wizara yake.

Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na Waziri Kivuli wa Fedha na Mipango, Mdee ni miongoni mwa wabunge waliompongeza Lukuvi kwa utendaji mzuri wa kazi.

Katika mahojiano na Nipashe nje ya Ukumbi wa Bunge mara tu baada ya bajeti ya wizara yake kupitishwa na chombo hicho cha kutunga sheria, Lukuvi aliwapongeza wabunge kwa kutambua juhudi zake.

"Nafikiri wabunge ndiyo wanajua sababu hasa ya kunipongeza na kuunga mkono bajeti ya wizara yangu, kina Mbowe nafikiri wanajua zaidi kuhusu," alisema.

"Kikubwa nawashukuru wabunge wote kwa 'ku-appreciate' (kuthamini) kazi ambayo ninafanya. Kama unavyojua, baada ya kuapishwa, ilibidi tuingie moja kwa moja kutekeleza kauli mbiu ya 'Hapa Kazi Tu' kwa vitendo.

"Kama ambavyo Mheshimiwa Rais amekuwa akisisitiza tuwatumikie Watanzania wote kwa haki bila kujali hali zao za kiuchumi, vyama vyao vya siasa.

"Wizara yangu inafanya kazi kwa kuzingatia hilo. Tunawahudumia Watanzania wote kwa haki."
Akichangia mjadala huo jana, Mbowe alimpongeza Lukuvi kwa uchapakazi wake na kuwataka mawaziri wengine kufuata nyayo zake.

Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), ndiye aliyekuwa mbunge wa kwanza wa upinzani kumpongeza Lukuvi juzi akilieleza Bunge kuwa mbunge huyo wa
Ismani (CCM) amefanya kazi nzuri anazozifanya katika wizara hiyo na baadaye wabunge wengine wengi wakiwamo wa upinzani wakaendelea kumwaga pongezi kwa uongozi wa wizara hiyo.

Kutokana na hali hiyo, Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya (Chadema), ambaye juzi alikuwa anakalia kiti cha Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alikiomba Kiti Cha Spika kitengue kanuni ili mjadala huo uhitimishwe jana saa 8:00 mchana badala ya saa 2:00 usiku.

Katika kujemga hoja yake, Bulaya alisema mjadala huo ulipaswa kuhitimishwa mapema kwa kuwa bajeti imeungwa mkono na pande zote mbili.

Mbunge huyo pia alisema haoni sababu ya kurefusha mjadala huo hadi saa 2:00 ilhali wabunge wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na upinzani walichangia kwa kuiunga mkono.

"Kwa kuwa bajeti hii imeungwa mkono na karibu wabunge wa vyama vyote, Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiomba Kiti kiruhusu kutengua kanuni ili kikao cha Bunge kesho (jana) kihitimishwe saa 8:00 mchana badala ya saa 2:00 usiku ili kutoa fursa kwa wenzetu Waislamu kuwahi kwenda kuungana na familia zao kuanza mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani," alisema.

Kutokana na ombi hilo, Mwenyekiti wa Bunge, Najma Murtaza Giga, alikubali kutengua kanuni na jana asubuhi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, alitoa hoja ya kutengua kanuni na wabunge wengi wakaridhia mjadala wa bajeti hiyo uhitimishwe saa 8:00 mchana.

Hata hivyo, upitishaji wa bajeti hiyo haukufika hata saa 8:00 mchana, kwani Bunge lilimaliza kazi hiyo saa 7:15 mchana.

Mbali na Mdee, wabunge wengine walimwagia pongezi Lukuvi kwa kazi nzuri, ni pamoja na Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Tarime Mjini (Chadema), Esther Matiko.

Wengine ni Joseph Hasunga (Vwawa-CCM), Anna Lupembe (Viti Maalum-CCM), Balozi Adadi Rajabu (Muheza-CCM), Rashid Shangazi (Mlalo-CCM), Shabani Shekilindi (Lushoto-CCM) na Abdallah Chikota (Nanyamba-CCM).

Mbali na kumpongeza Lukuvi, Shangazi na Shekilindi walimuomba waziri huyo kuwasaidia kumwondoa mwekezaji wa mradi wa shamba la katani katika Wilaya ya Lushoto ambaye anaendelea na uzalishaji licha ya kunyang'anywa ardhi kwa agizo la Rais.

"Kupimiwa ardhi Lushoto ni shida. Mwekezaji wa shamba la katani anadai ameishika serikali kama alivyosema Shangazi. Mtu huyu anatusumbua sana. Hatujui anajiamini kwa lipi. Nawaaminia sana watendaji wa wizara hii, naamini ninyi hamjashikwa," alisema Shekilindi.

Naye Chikota aliiomba serikali kuajiri watumishi wanaohitajika kutatua changamoto za ardhi nchini hasa jimboni kwake Nanyamba huku akimpongeza Rais John Magufuli kwa kuivunja iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Mkuu Dodoma.