Mawaziri wafanya ziara mpaka wa Tanzania na Uganda

Kagera. Mawaziri watano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wametembelea mpaka wa Tanzania na Uganda ili kutatua changamoto zinazoukabili mpaka huo na kuuboresha.

Mawaziri hao ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Suleman Jaffo.

Pia alikuwapo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Suzan Kolimba na Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Isack Kamwelwe.

Miongoni mwa maeneo yaliyotembelewa na mawaziri hao leo Alhamisi, Julai 27 ni eneo la mpaka ya Tanzania na Uganda kwa upande unapopita Mto Kagera na eneo la kivuko cha mpaka wa Tanzania na Uganda kilichopo Mtukula mkoani Kagera.

Katika ziara hii mawaziri hao wameweza kujionea hali halisi ya maisha ya wakazi wa mipakani na jinsi wanavyohusiana na wenzao wa nchi ya jirani ya Uganda ambapo wamekuwa wakishirikiana na kuishi kwa amani katika shughuli zao za kila siku.

Aidha, ziara hii ni maandalizi ya mkutano wa ujirani mwema kati ya mawaziri wa Serikali ya Uganda na mawaziri kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao unatarajiwa kufanyika Julai  29 , Bukoba mkoani Kagera.

Mwananchi: