Wastara atoa siri mpya


Msanii wa filamu nchini Wastara Juma ambaye sasa amepata shavu la ubalozi wa moja ya taasisi za kusaidia watu nchini Sweden amefunguka na kutoa siri ambayo ameishi nayo kwa zaidi ya miaka tisa bila kumweleza mtu.

Wastara akiwa kwenye kipindi cha KIKAANGONI ambacho kinafanyika kila siku ya Jumatano kupitia ukurasa wa facebook wa EATV amesema kuwa kipindi ambacho alikuwa akimuuguza mumewe marehemu Sajuki ndiyo kipindi ambacho alipatwa na majanga ya kupasua mguu wake wa bandia wakati akimfuatia mumewe chakula nje ya hospitali.

"Watu hawajui mimi wakati nampeleka Sajuki hospitali nilianguka barabarani na mguu niliokuwa nao ulinipasukia barabarani India wakati nashuka chini kwenda kumchukulia chakula Sajuki kwa siri maana alikataa chakula cha hospitali, nilikuwa sijawahi kushuka chini kwenye zile barabara maana sizijui wala sijui fujo zao kwani barabara za India zinafujo sana watu wanapiga sana honi utafikiri wanaenda harusini kwa hiyo zile kelele zilinichanganya akili nikaanguka katikati ya barabara na mguu ukanidondoka na kupasuliwa hapo hapo bahati nzuri nilikuwa na shemeji yangu akanibeba kama vile kanyakua kifaranga" alisema Wastara

Wastara amedaikuwa wakati yupo hospitali watu walikuja palepale hospitali na kumpima mguu kisha wakamtengenezea mguu mwingine kwa fedha ambazo alitumiwa na ndugu zake ambao wapo Omani Muscat kwani huko ndipo aliomba msaada.

"Hili jambo watu hawalijui na wala sijawahi kulisema sehemu kwani hapa ndiyo mara ya kwanza nalisema kwa hiyo kama mguu wangu naufanya ni mradi ningesema na kupiga picha ili mwisho wa siku watu wanichangie lakini sikusema sehemu kwa kuwa sifanya tatizo langu kama mradi" alisisitiza Wastara