Bakwata yatoa neno kuhusu kuandama kwa mwezi


Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kupitia kwa Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu yake, Sheikh Khamis Mataka, amesema kamati ya ufuatiliaji wa mwandamo wa mwezi ndiyo yenye mamlaka  ya kuutangaza.

Akizungumza na waandishi wa habari leo ofisi za BAKWATA jijini Dar es Salaam, Mataka amesema kuwa kesho Alhamisi Juni 29 ni siku ambayo mwezi utafuatiliwa, na ametaka umma wa Kiislamu kufuatilia na atakayeuona atoe taarifa kwa shehe wake au imamu wa msikiti wake ili mamlaka zinazohusika na kuutangaza ziweze kuujuza umma.

Pamoja na hayo amewataka Waislam kutopotosha taarifa za mwandamo wa mwezi ili kuondoa taharuki kwa umma.

Pia amesema kuwa Mufti Mkuu wa Tanzania, Shekh Abubakari Zubeir, amemshukuru Rais Magufuli kwa ziara yake ya jana ya kushtukiza katika ofisi za BAKWATA na kuhamasisha ujenzi wa msikiti wa baraza hilo ambapo alitoa mchango wake wa shilingi milion 10 ili kukamilisha ujenzi huo.