Atuhumiwa Kuwatorosha Wanafunzi na Kuwapeleka Dar Wakafanye Kazi za Ndani

Jeshi la Polisi mkoani Iringa linawashikilia watu wawili waliokuwa wakiwasafirisha wanafunzi watano wa shule ya sekondari ya Mlafu kwenda Dar es Salaam kufanya kazi za nyumbani.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Kamishna Msaidizi (ACP),  Juma Bwire, alisema  tukio lilitokea Julai 31, mwaka huu, katika mji mdogo wa Ilula, Kilolo mkoani Iringa.

Bwire alisema watuhumiwa hao walikuwa wakihangaika kuwasafirisha kwa ajili ya kuwatumikisha kazi za ndani, baada ya wanafunzi hao kutoweka kwa wazazi wao tangu Julai 29 mwaka huu na walisafirishwa kwa bodaboda kutoka Mlafu hadi Ilula.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Tulizo Mtega (19) na Rosemary Msasalage (18) wote wakazi wa Ilula na kwamba mbinu iliyotumika kuwarubuni wanafunzi hao ni kuwa wamepata kazi mbalimbali za kuuza maduka Morogoro na Dar es Salaam.