Diamond anavopata kismati cha wanawake wenye watoto


MARA nyingi wanaume wengi wanapenda kuwa wa kwanza kuwazalisha wanawake wanaokuwa nao kwenye uhusiano wa kimapenzi ili kuonekana wao ndiyo kidume lakini kwa bahati nzuri au mbaya, kwa mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amekuwa na kismati cha kuzaa na wanawake ambao tayari wameshazalishwa kabla.

Wanawake wengi ambao hawakuwa wamezaa kabla na kubanjuka na mkali huyu wa Bongo Fleva, licha ya kupendana sana na ‘kapo’ zao kupamba vyombo vya habari lakini mwisho wa siku, hawakubahatika kumzawadia Diamond mtoto. Japo suala la kuzaa linakwenda na mipango ya wahusika lakini kwa mapito yote ya ujana wake, Diamond hakuweza kupata mtoto na wanawake hao ambao hawajawahi kuzaa.

Pamoja na hayo, Diamond ni mwanamuziki ambaye alitamani sana kupata mtoto tangu kitambo na tena hamu ya kuwa na watoto ilizidi baada ya wacheza dansa wake wote kubahatika kupata watoto lakini yeye alikuwa bado na kuna wakati mwingine walikuwa wakimringishia watoto wao.

 LISTI YA DIAMOND
Kuna wanawake wengi warembo ambao Diamond alianza kutoka nao ikiongozwa na muigizaji Jacqueline Wolper ambaye mpaka sasa hivi hajapata mtoto. Penzi la Wolper lilitajwa kuwa la siri na hata hivyo halikudumu kivile, Diamond aliendelea na maisha yake mengine hata baadaye mmoja wa wasanii wa Kundi la Wasafi Classic Baby (WCB), Harmonize alijitwalia mrembo huyo lakini pia baadaye wakamwagana.

Huku na huku, Diamond akaingia kwenye himaya ya mrembo wa Tanzania, Wema Sepetu ambaye hapo naamini kabisa mwanamuziki huyo mpaka leo angetamani kupata naye mtoto lakini imeshindikana. Wawili hao walionekana kusaka mtoto kwa muda mrefu lakini hata hivyo haikuwezekana.

Warembo wengine ambao waliwahi kutoka na mwanamuziki huyu ambao walikuwa bado hawaijui ‘leba’ ni pamoja na mtangazaji Penniel Mungilwa ‘Penny’ ambaye huyu ilidaiwa alinasa ujauzito lakini ukachoropoka. Modo ‘mbichi’ Irene Hilary ‘Lynn’ ambaye pia alidaiwa kutembea na Diamond na kuleta mgogoro mkubwa kwenye uhusiano wake wa kimapenzi na mzazi mwenziye, Zarina Hassan ‘Zari’ naye hakuweza kuzaa naye.

KUTAMANI MTOTO KUMEMPONZA
Mwanamuziki huyo tangu awali alipokuwa ana uhusiano wa kimapenzi na Penny na Wema na wengineo ambao hawakuwa wamezaa kabla, alionekana alikuwa na shauku ya kupata mtoto lakini bahati haikuwa kwa warembo wa aina hiyo.

Kuonesha kwamba alikuwa na kiu ya kupata mtoto, alivyoanzisha uhusiano wa kimapenzi na Zari, hakujali sana suala la mrembo huyo wa Kiganda kuwa na idadi ya watoto aliozaa na mwanaume mwingine, alifurahia kitendo cha kupata mtoto na mwanamke huyo.

Diamond alimpa heshima zote Zari, kwa sababu ndiyo mwanamke wa kwanza kumpa mtoto licha ya kuwa mwanamama huyo tayari alikuwa na watoto wengine watatu, mwanamuziki huyo alikubali na kuwapenda watoto wote kama wanawe.

AIBUKIA KWA HAMISA
Baada ya kubahatika kumzalisha Zari watoto wawili, alianzisha uhusiano wa kisiri na mwanamitindo maarufu Hamisa Mobeto ambapo uhusiano huo ulizaa matunda na kumpata mtoto Dylan lakini tayari mwanamitindo huyo alikuwa ameshazalishwa mtoto mmoja huko nyuma.

ATATULIA WAPI?
Diamond ana kila sababu sasa ya kuchagua wapi kwa kutulia ili aweze kuwa na ndoa kwani tayari nyota yake ya kuzaa imeshajionesha kwa warembo tofauti ambao wote amewakuta na watoto wengine.

Bahati mbaya sana, uhusiano wake na Mobeto ulikufa baada ya kumuomba radhi Zari kwa kumsaliti akiwa kwenye uhusiano naye kisha akazaa na Mobeto kwa siri. Zari alimsamehe, wakaendelea na maisha yao lakini hata hivyo, Februari mwaka huu, boss lady huyo mwenye maskani yake nchini Afrika Kusini alitangaza kuachana na Diamond.

Hivyo, endapo kama Diamond atashindwa kurudiana na Zari aliyezaa naye watoto wawili na pia akashindwa kurudisha mpira kwa Mobeto aliyezaa naye mtoto mmoja basi atalazimika kutafuta mwanamke mwingine ambaye pengine atafunga naye ndoa. Pamoja na yote, bado atakuwa na jukumu la kuwalea watoto hao watatu aliowapata kwa mama tofauti, chaguo ni lake!