Jokate kuwavaa Wazazi, Walezi Wasiowapeleka Watoto Shule

Mkuu wa wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani, Jokate Mwegelo amesema atawachukulia hatua za kisheria wazazi au walezi wasiowapeleka watoto shule.

Alisema hayo juzi alipofanya ziara katika shule za msingi Chazige A na B alikokutana na wananchi na kusikiliza kero zao.

Jokate alisema mzazi au mlezi asiyempeleka shule mtoto hasa wa kike hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ikiwamo kupelekwa mahakamani.

Alisema wataendelea na kampeni ya “Tokomeza Ziro” yenye lengo la kukusanya fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu na miundombinu ya shule, madarasa na vyoo.

Naye ofisa elimu msingi wilayani Kisarawe, Shomari Bane alisema: “Kampeni imetusaidia, wanafunzi kuanzia mwaka jana ufaulu darasa la saba uliongezeka na walifanya vizuri.

Pia, Jokate alimuagiza mganga mkuu na madaktari wilayani Kisarawe kutoa dawa zilizopo hospitalini kwa wagonjwa na kama hazipo, watoe mbadala ili wananchi wasipate usumbufu.