UN yammwagia pongezi Kabila kwa kutogombea tena


Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limepongeza uamuzi wa Rais Joseph Kabila kutowania muhula mwingine katika uchaguzi ujao wa DRC, na kusema uchaguzi huo unapaswa kupelekea makabidhiano ya amani ya madaraka.

Baraza hilo pia limevihimiza vyama hasimu vya siasa nchini humo, pamoja na taasisi zinazohusika na maandalizi ya uchaguzi huo wa mwezi Desemba, kuhakikisha kuwa zoezi la upigaji kura linakuwa la amani na la kuaminika.

Baraza hilo ambalo ndiyo chombo chenye nguvu zaidi ndani ya Umoja wa Mataifa kilitoa taarifa jana Jumatatu na kukaribisha hatua za karibuni katika mchakato wa uchaguzi, ikiwemo ya Rais Joseph Kabila kutimiza ahadi yake ya kuheshimu katiba ya Congo kwa kutowania muhula wa tatu.

Wanachama wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa waliwahimiza washiriki wote kuhakikisha kuwa uchaguzi huo unafanyika katika mazingira ya uwazi, uaminifu na ushirikishwaji. Walisema kuheshimu haki za msingi na kusimamia kalenda ya uchaguzi ni mambo muhimu yatakayohakikisha uchaguzi wa amani hapo Desemba 23.

Kabila ambaye amekuwa madarakani tangu mwaka 2001, alionekana kusalimu amri kwa shinikizo la kimataifa wiki iliyopita, wakati muungano wake tawala ulipomteuwa Emmanuel Ramazani Shadary kuwa mgombea wake wa nafasi ya rais katika uchaguzi wa mwaka huu.