Serikali yasema Majibu ya typhoid, U.T.I mengi ya uongo


SERIKALI imesema majibu mengi ya vipimo vya maradhi ya tumbo (typhoid) na maambukizi kwa njia ya mkojo (U.T.I) yanayotolewa na maabara mbalimbali nchini ni ya uongo.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile, alipohojiwa na kituo kimoja cha televisheni.

Dk. Ndugulile alisema magonjwa ya typhoid na U.T.I, majibu ya vipimo vyake havipatikani kwa saa mbili au siku moja.

Asilimia 70 ya homa ni virusi ambavyo tunavipata baada ya saa tatu au saba vinapotea,” alisema na kuongeza:

“Watu wengi wanakwenda maabara wanasema wanasikia homa au viungo vinauma au mwili uko ovyo, wanaambiwa una malaria…Hii si kweli kwa sababu malaria ni kidogo sana na kwa sasa hivi wastani wa taifa ni asilimia 14 pekee ya watu wanaougua malaria,” alisema.

Alisema majibu ya vipimo vya U.T.I na typhoid kwa kawaida huchukua hadi muda wa saa 72, lakini cha kushangaza kwenye maabara nyingi huchukua chini saa mbili.

“Ukitaka kupima typhoid kitaalamu unatakiwa kuchukuliwa damu iende maabara ikapandikizwe, ije iangaliwe vimelea vilivyoota...majibu haya yanachukua saa 72, si muda mfupi kama tunavyoshuhudia kwenye maabara nyingi,” alisema na kuongeza:

“Juzi kuna msichana alipewa dawa nne, hii si sahihi, mtu anachokifanya anapiga risasi zote kwa kutaka kuua sisimizi, lakini kama una homa unakwenda kwa daktari anakuandikia dawa ya malaria, dawa ya kupunguza homa, Antibiotic na dawa ya kuchua, jua huyo siyo daktari, huyo ni mganga wa kienyeji,” alisema Naibu Waziri.