Uongozi wa Klabu ya Simba umesema kuwa haujapokea taarifa ya kusimamishwa kwa mchakato wa Uchaguzi wao ambao unaendelea hivi sasa.
Ofisa Habari wa klabu hiyo Haji Manara ameyasema hayo Leo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam, amesema mpaka sasa hawana taarifa rasmi juu ya kusimamishwa kwa mchakato huo ambapo zoezi la urudishaji fomu limeshakamilika.
Manara ameeleza kutokusimama kwa mchakato huo kwa sababu hawana barua rasmi kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) hivyo utaendelea kama kawaida.
Ikumbukwe juzi Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi TFF, Wakili Msomi Revocatus Kuuli, alisema wameupiga 'STOP; mchakato huo akieleza Simba wamekiuka baadhi ya vipengele vya katiba ya wanachama wa TFF.
Kuuli alisema moja ya mambo yaliyosababisha kusimamishwa kwa mchakato huo ni ongezeko la ada ya uanachama kwa wagombea nafasi ya Uenyekiti na ngazi ya Ujumbe.
