Taifa Stars ya Amunike usipime, yafufua matumaini ya Cameroon


CHEREKO! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' kuichapa bila huruma Cape Verde kwa mabao 2-0 katika mchezo wa kuwania kufuzu michuano ya mataifa Afrika nchini Cameroon mwakani.

Stars inayonolewa na staa wa zamani wa Barcelona na Timu ya Taifa ya Nigeria, Emmanuel Amunike imepata ushindi huo kufuatia magoli yaliyofungwa kila kipindi na mastaa wake wanaocheza soka la kimataifa, Simon Msuva anaecheza Morocco akifunga goli la kwanza huku Nahodha Mbwana Samatta 'Poppa' akifunga goli la pili.

Samatta ambaye anakipiga Genk ya Ubelgiji inayoshiriki pia michuano ya Europa angeweza kuipa Stars goli baada ya mkwaju wake aliopiga kugonga mwamba kabla ya dakika chache mbele kutengeneza goli la kuongoza lililofungwa na Msuva.