Muungano wa Afrika AU umeiomba Congo iahirishe kutangaza matokeo ya uchaguzi


Muungano wa Afrika (AU) umeitaka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo iahirishe kutangaza matokeo ya uchaguzi mkuu.

Muungano huo unaonuia kuhimiza umoja na demokrasia, unasema una "shaka kubwa" na matokeo ya awali yaliotangazwa wiki iliyopita, Matokeo hayo yalimpa ushindi mgombea wa upinzani Felix Tshisekedi lakini mpinzani wa utawala uliopo, Martin Fayulu, anasisitiza kuwa yeye ndiye aliyeshinda.

Kumezushwa maswali mengi kuhusu uhakika wa matokeo hayo huku kukiwepo shutuma kwamba Tshisekedi anapanga mpango wa kugawana madaraka na rais anayeondoka Joseph Kabila.

Baadhi ya viongozi katika Muungano wa Afrika na Serikali walikutana katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa jana Alhamisi na kutoa tamko kuhusu Uchaguzi huo wa Desemba 30 unaopingwa pakubwa.

"Kumekuwa na shaka kubwa kuhusu namna matokeo ya awali yalivyokusanywa, kama ilivyotangazwa na tume huru ya kitaifa ya uchaguzi kwa kura zilizopigwa," taarifa ya muungano huo imesema.

Hata hivyo AU imetaka kuahirishwa kutangazwa kwa matokeo ya mwisho ya uchaguzi mkuu huo, Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kutangazwa leo Ijumaa.