https://monetag.com/?ref_id=TTIb Zitambue faida za kunywa maji ya madafu | Muungwana BLOG

Zitambue faida za kunywa maji ya madafu


Huenda ulikuwa hujui lakini kwa sasa unapaswa kufahamu kuwa maji ya dafu ni muhimu kwa mwili wa binadamu, kwa sababu huimarisha kinga ya mwili.

Lakini unaweza kujiuliza kwa nini maji ya madafu yanapendwa sana na baadhi ya watu. Jibu ni moja tu, licha ya kinywaji hicho kuburudisha na kupunguza hali ya uchovu wa mwili lakini pia kwa wale wenye mning’inio wa pombe (hangover) huwasaidia kuondosha hali hiyo.

Pia, husaidia kuua bacteria wa aina mbalimbali wakiwamo wale wanaosababisha maambukizi kwenye njia ya mkojo yaani UTI.

Wataalamu wa masuala ya lishe wanasema maji ya dafu husaidia pia kupunguza maumivu wakati wa kupata haja ndogo (mkojo).

Pamoja na faida hizo, maji haya huongeza virutubisho vya aina tano na vyote huwa na umuhimu ndani ya mwili wa binadamu.

Virutubisho hivyo ni pamoja na Calcium, magnesium, potassium, phosphorus na sodium, ambavyo ni muhimu katika mwili wa binadamu.

Unywaji wa maji ya madafu mara kwa mara husaidia kupunguza tatizo la msukumo mkubwa wa damu mwilini. Wataalamu wa lishe wanashauri maji hayo yanywewe asubuhi kabla ya kutumia chakula au kinywaji chochote.

Kwa watu wanene, matumizi ya dafu huwasaidia kupunguza uzito na kuwaongezea hamu ya kula kutokana na uasilia wake.

Mbali na watu wanene, pia wataalamu wa lishe wanasema ulaji wa madafu una faida kubwa hata kwa watu wanaocheza michezo mbalimbali, kwani huwasaidia kuwaondolea uchovu na kuwaongezea nguvu wawapo uwanjani.

Hivyo, inashauriwa kila mmoja kutumia dafu kwani lina faida lukuki ndani ya mwili wa binadamu.