Waganga wa Jadi Njombe kuhakikiwa kuwabaini wauaji wa watoto


Kufuatia mauaji ya watoto yaliyotokea siku za hivi karibuni mkoani Njombe, Serikali mkoani
humo imeanza kufanya uhakiki wa waganga wa tiba asilia ikiwa ni mchakato wa kuwasaka waganga
wapiga ramli.

Hatua hiyo inakuwa zikiwa ni siku kadhaa baada ya Watoto sita, wakiwemo watatu wa familia moja
wenye umri chini ya miaka 10 kupatikana wakiwa wamefariki katika mazingira ya kutatanisha mkoani humo.

Hivi karibuni Bungeni Waziri wa Mambo ya Ndani Kangi Lugola alitoa tamko la serikali kuhusu
mauaji ya watoto yanayoendelea mkoani humo.

Alisema kuwa tayari watu 29 wanashikiliwa na jeshi hilo na tayari timu ya wapelelezi imetumwa
mkoani humo kuvisaidia vyombo vya dola kuchunguza matukio hayo kwa kutumia falsafa ya ulinzi shirikishi.