Fiada za kufanya kazi kwa bidii

Kuna fikra potofu zimejengeka miongoni mwa watu wakidhani kuwa kufanya kazi kwa bidii ni utumwa. Hii ni kutokana na dunia ya sasa kujaa watu wasiopenda kazi na wavivu.

Kwa hakika kufanya kazi kwa bidii kuna manufaa mengi sana ambayo watu wengi hawayajui. Huu ni wakati wa kubadili mtazamo wako juu ya kufanya kazi kwa bidii kwa kufahamu faida  za kufanya kazi kwa bidii.

1. Utaweza kutumia muda vyema
Huwezi kutumia muda vyema kama hutofanya kazi kwa bidii. Ukiwa na bidii katika kufanya kazi, unaweza kufanya kazi za siku nzima ndani ya saa moja au kazi za siku mbili ndani ya siku moja.

Hakuna mtu yeyote aliyefanikiwa bila kutumia muda vyema, muda ni mali hivyo yakupasa uutumie vyema kwa kufanya kazi kwa bidii.

2. Kufikia malengo yako
Kanuni moja wapo ya kufikia malengo ni kufanya kazi kwa bidii. Safari ya mafanikio siyo ya mteremko, inahitaji juhudi nyingi ili tuweze kuona matokeo.

Hakuna mtu aliyewahi kufanikiwa kwa kufanya kazi kivivu, fuatilia watu waliofanikiwa watakueleza jinsi wanavyofanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha ndoto zao.

3. Kuheshimika
Nani atamheshimu mvivu? Kwa hakika hakuna. Mtu anapokuwa mwenye bidii utasikia kauli kama vile huyo hapendi mchezo, akishaingia kwenye kazi zake humpati, hageukagi nyuma kwenye kazi huyo, kama huyo yupo hiyo kazi lazima iishe, n.k.

Hizi ni baadhi ya kauli zinazoonyesha kuheshimiwa kwa mtu husika kutokana na kufanya kazi kwa bidii. Ikiwa unataka kuheshimika ni lazima ufanye kazi kwa bidii.

4. Kutambulika
Ikiwa unafanya kazi kwa bidii huna haja ya kujikombakomba kwa wakubwa au mbele za watu ili utambulike; bidii yako ya kazi itakutambulisha.

Naamini umewahi kusikia watu wakipewa tuzo kwenye sherehe za kitaifa kutokana na kufanya kazi kwa bidii; hili linatupa picha ya kipekee ya faida ya kufanya kazi kwabidii.

Usijali hata kama wanakudharau au wanakuona duni, wewe fanya kazi kwa bidii watakutambua ukiwepo au hata wakati utakapoondoka wataona pengo lako.

5. Kuondoa lawama na manung’uniko
Mara nyingi idara au ofisi zenye malalamiko mengi ni zile zenye wafanyakazi wavivu. Pia wafanyakazi wengi wanaolaumiwa na kunyoshewa vidole na waajiri wao, wengi ni wale wavivu.

Ili kuepuka lawama au manung’uniko, ni vyema ukafanya kile unachokifanya kwa bidii kwani kwa njia hii utaongeza ufanisi wako.

6. Kupata matokeo makubwa
“Kazi kubwa = Matokeo makubwa.”

Hakuna matokeo makubwa bila kazi kubwa, yaani kazi iliyofanywa kwa bidii. Kwa mtu yeyote anayetaka kuona matokeo makubwa katika kile anachokifanya ni lazima kwanza afanye bidii.

Kumbuka hata mkulima anayefanya bidii katika kilimo ndiye huvuna zaidi ya wakulima wengine. Hivyo kufanya kazi kwa bidii hakuepukiki kwenye maisha.

7. Huleta fursa mpya
Mtu mwenye bidii kila mara hufungua milango ya kupata fursa mpya, kazi zake na bidii yake humtangaza na kumfungulia fursa zaidi. Hakuna mtu atakayempa mtu mvivu kazi au fursa zenye manufaa.

Hapa nakumbuka mfano wangu binafsi kwenye kazi ya mwezi mzima niliyoifanya usiku na mchana bila kuchoka kwa wiki mbili pekee. Kazii hii ilinipa sifa njema na kuniwezesha kupata kazi nyingine lukuki.

8. Kuboresha afya
Kukaa bila kufanya kazi ni kujiletea matatizo ya kiafya; kazi ni sehemu ya mazoezi. Hivyo kufanya kazi kwa bidii kutakufanya uwe mwenye afya njema kila wakati.

Unalotakiwa kukumbuka hapa ni kuwa na kiasi, fanya kazi kwa bidii lakini usipitilize hadi uathiri afya yako.

Kwa hakika mkono wa mtu mwenye bidii hauwi mtupu. Mtu mwenye bidii hujitesa kwa muda mfupi lakini matokeo yake huwa ni mazuri na ya muda mrefu.

Haipingiki kuwa bidii ndiyo kanuni mojawapo ya mafanikio.

Kumbuka hakuna mkato kwenye mafanikio; mtangulize Mungu, weka malengo, fanya bidii na matokeo ni hakika.