Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ampongeza Rais Magufuli


Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema nchi yake itaendelea kukuza ushirikiano kati yake na Tanzania na hasa kuimarisha uchumi.

Ahadi hiyo ilitolewa katika mazungumzo kwa njia ya simu na Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

 Angela Markel amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa zinazofanywa katika kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji ikiwemo kupambana na rushwa na kuimarisha miundombinu.

 Angela Markel ameahidi kuwaleta wafanyabiashara watakaowekeza katika maeneo mbalimbali ikiwemo kujenga kiwanda cha kuzalisha mbolea ambacho kitakuwa kikubwa kuliko vyote barani Afrika lengo likiwa kukuza juhudi za ujenzi wa viwanda nchini na hivyo kuongeza pato la nchi.

Ametoa wito wa kuimarishwa kwa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) na amemwalika kwa mara ya pili Rais Magufuli kutembelea Ujerumani, ziara ambayo itatanguliwa na ziara ya Mawaziri wa Tanzania kukutana na Mawaziri wa Ujerumani.

Kwa upande wake Rais Magufuli amemshukuru Angela Merkel kwa kumpigia simu na kueleza dhamira yake ya kukuza zaidi uhusiano wa Tanzania na Ujerumani na amebainisha kuwa Tanzania itahakikisha inajenga mazingira mazuri katika maeneo yote ya ushirikiano yakiwemo biashara na uwekezaji.