Agizo la Rais Magufuli kukamilishwa kituo cha Mabasi Njombe ndani ya siku 30 haliwezi kufanikiwa


Na. Amiri kilagalila-Njombe

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa  Njombe,  Edwirn Mwanzinga amesema kuwa maendeleo ya ujenzi wa kituo kipya cha mabasi cha Njombe mjini yanaashiria kuwa kituo hicho hakita weza kukamilika kwa asilimia 100 ndani ya muda walioagizwa na Rais Magufuli.

Mwanzinga amesema hayo hii leo ikiwa ni Wiki moja imepita tangu Rais Magufuli kuagiza kituo cha mabasi kinachoendelea kujengwa mkoani Njombe kukamamilika ndani ya siku 30 tangu april 10  mpaka mei 10 mwaka huu.

Itakumbukwa kwamba kutokana na ujenzi kutumia muda mrefu bila kukamilika akiwa katika ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Njombe Aprili 7-9, Rais Magufuli aliagiza Wizara ya Ujenzi  kwa kushirikiana na Halmashauri ya Mji wa Njombe kukamilisha ujenzi ndani ya siku 30.

Akizungumza na Muungwana Blog,  Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Njombe,  Edwirn Mwanzinga amesema kuwa baadhi ya shuguli zinazoendelea katika kituo hicho cha mabasi haziwezi kuwa zimekamilika ndani ya muda huo wa siku thelathini  kutokana na ukubwa wa kazi huku  hali ya hewa ikiwemo mvua pia ikiathiri kazi hiyo.

"Tuna kazi mbili pale katika kituo cha mabasi kipya tunachoendelea kujenga, ni ujenzi katika eneo la kupaki magari madogo ambapo mkandarasi alikuwa anashindwa kutandika peving bloks kutokana na tope linalotokana na mvua nyingi’’alisema Mwenyekiti Halmashauri ya Mji Njombe.

Amezitaja baadhi ya kazi ambazo zinaendelea katika kituo hicho kuwa ni pamoja na utoaji wa kifusi,ujenzi wa parking za maeneo ya kukatia tiketi,pamoja na maeneo ya kupumzika abiria ambayo yanahitaji kumiminwa kwa zege na ufungaji wa milango na mageti.

Mwanzinga aliongeza kuwa licha kazi kubwa ya ujenzi kukamilka mpaka kufikia mei 10,2019 lakini  kituo hicho hakitaanza kutumika  ili kuwezesha shughuli zote kukamilika ambapo amesema halmashauri inatarajia kuanza kukitumia kituo hicho rasmi mapema julai ,2019 utakapo anza mwaka wa fedha.

"Hata kama mkandarasi akikamalisha kazi zote ndani ya muda tuliopangiwa na mh Rais lakini hatutaweza kuruhusu kituo kuanza kutumika kwa sababu maduka yaliyopo pale yatakuwa bado kuanza kutumika kwa kuwa bado hatuja pata wafanyabiashara katika vibanda ‘’ aliongeza Mwanzinga

Ujenzi wa kituo hicho cha mabasi unatarajia Kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 9 na ulianza kujengwa  tangu mwaka 2013 huku ukijengwa kwa awamu tatu ambapo katika awamu ya mwisho unagharimu zaidi ya shilingi bilioni 5.7