Mfanyakazi wa huduma za afya auawa DRC


Mfanyakazi mmoja wa huduma za afya aliyekuwa akihudumia wagonjwa wa Ebola amepigwa risasi na kuuawa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

 Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema kuwa daktari huyo, raia wa Cameroon, aliuawa kwenye mji wa mashariki wa Butembo hapo jana.

Mkuu wa shirika hilo, Tedros Adhanon Ghebreyesus, amethibitisha kifo cha mfanyakazi huyo kupitia ujumbe wake wa Twitter.

Meya wa mji wa Butembo, Sylvain Kanyamanda, amesema mauaji yalifanyika kwenye Kliniki ya Chuo Kikuu ya Butembo, akiwatuhumu waasi wa kundi la Mai-Mai kuhusika.

Mashambulizi dhidi ya wafanyakazi wa huduma za afya kwenye eneo hilo, ambalo WHO inasema limeshapoteza watu 751 kwa Ebola, yamekuwa yakifanyika mara kwa mara.