Umoja wa Afrika waonya mapinduzi ya kijeshi Sudan


Umoja wa Afrika (AU) umetishia kuisimamisha Sudan kufuatia mapinduzi ya wiki iliyopita yaliyoshuhudia Omar al-Bashir akiondolewa madarakani na jeshi.

Katika taarifa yake Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika, limesema ikiwa jeshi litashindwa kukabidhi madaraka kwa raia ndani ya siku 15, basi Umoja wa Afrika utasitisha ushiriki wa Sudan katika shughuli zote za Umoja huo hadi pale amri ya kikatiba itakaporejeshwa.

Bashir ameitawala Sudan kwa miaka 30 kabla hajaondolewa wiki iliyopita kufuatia maandamano ya nchi nzima yaliyoanza mwezi Desemba.

 Hata hivyo Umoja huo umesifu madai ya waandamanaji na kuita uingiliaji wa jeshi kuwa ni mapinduzi ambayo umeyalaani.

Umoja wa Afrika ulio na wanachama 55 umeongeza kuwa serikali ya mpito ya kijeshi itakuwa ni tofauti matakwa ya watu wa Sudan. Umoja huo umekuwa na msimamo mkali kuhusiana na mapinduzi na uliwahi kuzisimamisha Misri na Jamhuri ya Afrika ya Kati mwaka 2013 kufuatia mapinduzi katika nchi hizo mbili.