Mwalimu wa shule ya msingi akutwa na AK 47


Na Rashid Nchimbi

Mtu mmoja aitwaye Solomon Letato Kipuker (30) ambaye ni Mwalimu wa shule ya Msingi Naan iliyopo kata ya Enguserosambu tarafa ya Loliondo wilayani Ngorongoro amekatwa akiwa na silaha aina ya AK 47 ikiwa na risasi Tano ndani ya Magazine.

Akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake leo asubuhi Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Jonathan Shanna, amesema kwamba tukio hilo limetokea Juni 2 mwaka huu baada ya Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa kushirikiana na Kikosi Kazi cha kupambana na uhalifu hasa ujangili kupata taarifa za Kiintelijensia na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo.

“Mtuhumiwa huyo ni miongoni mwa wafanyabiasahara haramu wa nyara za Serikali ikiwemo meno ya Tembo ambapo mara baada ya kumhoji alikiri kumiliki silaha hiyo kwa kushirikiana na wenzake ambao bado Jeshi la Polisi tunawatafuta”. Alifafanua Kamanda Shana.

Aidha Kamanda Shana alisema kwamba, mtuhumiwa huyo alikiri pia kujihusisha na ukodishaji wa silaha hiyo katika matukio mbalimbali ya kiuhalifu hasa utekaji ambayo yalishawahi kutokea wilayani humo kipindi cha nyuma.

Hata hivyo Kamanda Shana alimpongeza Kamishna wa Uhifadhi (TANAPA) Dkt. Allan Kijazi kwa kuzidi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kupambana na matukio mbalimbali ya uhalifu ndani ya mkoa huu wa Arusha.

Katika Operesheni zinazoendelea kila siku ndani ya wilaya zote sita za mkoa huu, Mei 30 mwaka huu, Jeshi hilo lilifanikiwa kuwakamata watu watatu (Majina yamehifadhiwa) wakiwa na jumla ya vipande vinne vya Meno ya Tembo katika Kata ya Maji ya Chai tarafa ya King’ori wilayani Arumeru na wanatarajiwa kufikishwa Mahakamani hivi karibuni.