CWT Dodoma, Mavunde wawataka Watanzania kutembelea vivutio vya utalii

Chama cha Walimu (CWT) Jiji la Dodoma kimewataka Watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya Utalii ili kukuza Utalii wa ndani hapa nchini Tanzania katika kumuunga Mkono Rais Dr John Pombe Joseph Magufuli kwenye azma yake ya kuhakikisha sekta ya Utalii inakua na kuchangia pato la Taifa na kuliingizia Taifa fedha nyingi za kigeni.

Hayo yamesemwa na Katibu wa CWT Wilaya ya Dodoma Mjini, Kelvin Mahundi kwa niaba ya walimu wenzake wakati wa ziara fupi ya Mafunzo katika Kituo cha Mali kale cha Michoro ya Miambani Wilayani Kondoa-Dodoma ambapo walimu hao kwa umoja wao walimshukuru Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, Mhe Anthony Mavunde kwa kugharamia ziara yao ambapo wamewataka Watanzania kuonesha uzalendo kwa kutembelea vivutio vilivyopo nchini.

Kwa upande wake Mhe Mavunde ameungana na walimu hao kutoa wito kwa Jamii ya Watanzania kujiwekea utaratibu wa kutembelea vivutio vya Utalii kama ambavyo yeye aliona umuhimu wa kuwapeleka walimu wa Jiji la Dodoma kwenda kujifunza mambo ya Mali kale katika Michoro ya miambani-Kolo Kondoa.


"Hapa Kolo,Kondoa ni eneo zuri la kujifunza kuhusu historia na utamaduni wa jamii ya watu wanaoishi eneo hili kupitia hapa Kituoni.Awamu ya kwanza niliamua kuwaleta walimu na awamu ya pili sasa nitawaleta wanafunzi ili waje wajifunze nao pia.Nitaendelea kuwa Balozi mzuri katika kuhamasisha watu waje waone urithi huu wa Dunia kupitia michoro ya kwenye miamba hapa Kolo-Kondoa"Amesema Mavunde.