F Faida za kupanga ratiba yako binafsi | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

Faida za kupanga ratiba yako binafsi

Ratiba siyo muhimu tu kwa ajili ya taasisi fulani pekee; ni muhimu pia kwa mtu binafsi. Watu wengi hushindwa kutumia muda wao vyema kutokana na kutokuwa na ratiba nzuri inayoeleweka.

Kuweka ratiba kutakuwezesha kupangilia kazi na mipango yako kwa namna ambayo utaweza kuitekeleza vyema.

Ikiwa unataka kuwa mwenye tija na ufanisi zaidi, basi fahamu faida  za kuwa na ratiba binafsi;

1. Kutumia muda vyema
Moja kati ya manufaa makubwa ya kuwa na ratiba ni kuweza kutumia muda vyema. Unapokuwa na ratiba ni vigumu kupata muda ambao haujapangiwa jukumu au kazi kwenye ratiba.

Unapokuwa na ratiba muda wako wote utatumika vizuri tena kwa shughuli yenye tija iliyopangwa. Hivyo ni vyema kuhakikisha unajiwekea ratiba na unaifuata ipasavyo.

2. Kuweka vipaumbele
Kuweka ratiba ni mbinu mojawapo ya kuweka vipaumbele. Unapoweka ratiba ni lazima utaondoa mambo yasiyo ya msingi ili ratiba yako ikae vyema na itekelezeke.

Kwa kujiwekea ratiba nzuri utaondoa mambo ambayo kimsingi hayakuwezeshi kufikia malengo yako. Kwa mfano huwezi kuweka muda wa kuchat kwenye ratiba.

3. Kuongeza ufanisi
Kufanya vitu bila mwongozo au mpangilio hukufanya ukose ufanisi. Kwa kuwa na ratiba utaweza kuwa na kitu kinachokuongoza na kukupa mpangilio mzuri.

Mana siku inapoanza unakuwa tayari umeshafahamu unaaza na nini na kinafuata nini badala ya kushika hiki na kile.

4. Kutokusahau mambo
Ni vigumu sana kusahau jambo ambalo lipo kwenye ratiba yako. Hii ni kutokana na sababu kuwa unafanya kazi kwa kufuata ratiba, kila mara utakuwa unatazama ratiba yako inataka ufanye nini na kwa muda gani.

Unaposahau mambo unayotakiwa kuyafanya, unapaswa kurejea kwenye ratiba yako na kutazama inataka ufanye nini.

5. Kupata muda wa kupumzika
Watu wengi wanakosa muda wa kupumzika kwa sababu wanafanya hiki mara kile bila mpangilio maalumu. Hili huwafanya kuhangaika siku nzima bila hata kujua wamekamilisha nini.

Utamsikia mtu akisema “leo nimechoka sana hata sijui nimefanya nini” “leo nahangaika tu hata hamna nilichofanya”. Hii inaonyesha kuwa mtu huyu amechoka bila hata kukamilisha kazi zake.

Kwa kujiwekea ratiba utaweza kupanga muda wa kazi na muda utakaoutumia kwa ajili ya kupumzika.

Kwa hakika hatuwezi kufanya mambo yafanikiwe na kwa wakati ikiwa hatutakuwa na ratiba nzuri tunayoifuata kikamilifu. Ni muhimu ukatenga muda ukaanda ratiba yako ya siku, wiki au hata mwezi.