Korea kaskazini yaishutumu Korea kusini kuhusiana na ununuzi wa ndege za kivita

Korea kaskazini imeishutumu Korea kusini kuhusiana na ununuzi wa ndege za kivita zenye uwezo mkubwa chapa F-35 kutoka Marekani, ikionya leo kuwa itajibu kwa kutengeneza silaha zake maalum za kuharibu ndege hizo.

Taarifa hiyo ambayo pia imeitaka Korea kusini kuachana na kile ilichokiita fikira za kipuuzi ili kuboresha mahusiano, inakuja wakati Korea kusini imeeleza matumaini kuwa mkutano wa hivi karibuni kati ya rais Donald Trump na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un utasaidia kufufua mazungumzo kati ya Korea hizo mbili.

Kwa ununuzi wake mkubwa kuliko yote wa silaha, Korea kusini inataka kununua ndege za kivita 40 chapa F-35 kutoka Marekani hadi ifikapo mwaka 2021. Ndege mbili za kwanza zimewasili mwezi Machi na mbili zaidi zitakabidhiwa nchi hiyo katika wiki mbili zijazo.