Ratiba ya Ligi ya Mabingwa Afrika yatoka, Simba SC na Yanga SC kuanza hivi


Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) limetoa ratiba ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika (CAFCL) msimu ujao wa 2019/20 ambapo wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano hiyo Simba na Yanga wamepangwa kuanza na timu kutoka katika ukanda wa COSAFA (Kusini mwa Afrika).

Mabingwa wa Tanzania Bara Simba SC wamepangwa kuanza na UD do Songo ya Msumbiji na wataanzia ugenini huku Yanga walioshika nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita wakipangwa kuanzia nyumbani dhidi ya Township Rollers ya Botswana.

Kwa mujibu wa ratiba, mechi za kwanza za raundi ya kwanza zitapigwa kati ya Agosti 9, 10 na 11 huku mechi za marudiano zikipigwa kati ya Agosti 23, 24 na 25.

Endapo vigogo hao wa Tanzania watapenya kwenye hatua hiyo, wataingia kwenye raundi ya pili ambapo Simba itakutana na mshindi kati ya Nyasa Big Bullets dhidi ya FC Platinum huku Yanga ikikutana na mshindi kati ya Green Mamba dhidi ya Zesco United.

Mechi za raundi ya pili zitapigwa kati ya Septemba 11, 13 na 14 na marudiano itakuwa ni kati ya Septemba 27. 28 na 29.