Mkutano wa Zitto Kabwe wazuiwa


Polisi Kanda Maalim ya Dar es Salaam wamezuia mkutano wa waandishi wa habari na Kiongozi wa ACT Wazalendo, Zitto Kabwe ambao ulitarajiwa kufanyika leo Ijumaa.

Polisi waliwasili Makao Makuu ya chama hicho na gari wakiwa wamevaa nguo za kiraia na kuzuia mkutano huo. Baadaye gari ya polisi walio na sare waliwasili na kumhitaji kiongozi yoyote wa chama.

"Ndugu waandishi huu mkutano usubiri kwanza, kwa hiyo ninawaomba mtawanyike mara moja," amesema askari mmoja aliyejitambulisha kama RCO wa Kinondoni, John Malulu.

Wakati waandishi wakitawanyika aliwasili Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano wa ACT Wazalendo, Ado Shaibu ambaye walimchukua kwa ajili ya mahojiano.

Hata hivyo, kabla ya kuchukuliwa na polisi, Ado Shaibu alisema polisi walikwenda nyumba kwa Zitto kumtafuta kwa ajili ya kumhoji.