Mtoto auwawa kwa kuliwa na Simba


Mtoto mmoja wa kike aliyejulikana kwa jina la Kangwa Manuga (6) mkazi wa kitongoji cha Sitobwike katika kijiji cha Sitalike Halmashauri ya Nsimbo mkoani Katavi ameuwawa kwa kuliwa na simba wakati amelala na mama yake katika kibanda kisichokuwa na mlango karibu na zizi la ng’ombe.


Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari Kamanda wa Polisi mkoa wa Katavi Benjamin Kuzaga amesema tukio hili limetokea usiku wa tarehe moja mwezi huu majira ya saa nane usiku.

Amesema Simba huyo aliingia katika kibanda walichokuwa wakiishi ambacho hakina mlango na kiko karibu na zizi la Ng’ombe na kisha kumnyakua mtoto na kumburuzia nje ambapo alimla mtoto huyo na kubakiza fuvu la kichwa na mifupa ya miguu.

Hili ni tukio la tatu kutokea katika kijiji kilichopakana na hifadhi ya Taifa ya Katavi tangu mwaka huu uanze; ambapo katika tukio la kwanza mtu mmoja alijeruhiwa na simba wakati tukio la pili mtu mwingine aliuwawa hivyo Kamanda huyo wa Polisi mkoa wa Katavi ametoa wito kwa wananchi kuacha kuishi katika maeneo ya karibu na hifadhi.

”Nawashauri wananchi wanaoishi ndani au kandokando ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi watoke na kwenda maeneo mengine ili kujiepusha na maafa yasiyo ya lazima,” alisema Kamanda Kuzaga.

Katika tukio jingine Polisi wamemkamata mtu mmoja Emmanuel Lukanda (28) mkazi wa kitongoji cha Mabambasi  kijiji cha Chamaland katika Halmashauri ya Mpimbwe akiwa na meno matatu ya tembo

Mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa njiani akisubiria wateja .Polisi wamesema wanamshikilia na kuendelea kumhoji kuhusu mtandao wa majangili wanaoharibu rasilimali za Taifa.

Aidha Kamanda huyo wa Polisi mkoa wa katavi ametoa rai kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano ili kukabiliana na wahalifu na kulinda rasilimali za nchi.